Thursday, March 28, 2013

UEFA YATAKA MAREFA WASIMAMISHE MECHI MARA MOJA IKIWA KUTATOKEA VITENDO VYA UBAGUZI KUTOKA KWA MASHABIKI JUKWAANI AU KWA WACHEZAJI UWANJANI…!

Kevin-Prince Boateng (namba 10) akitoka uwanjani baada ya kukerwa na vitendo vya ubaguzi wa rangi.
SOFIA, Bulgaria
Shirikisho la Soka la Ulaya (UEFA) limependekeza kwamba marefa wasimamishe mechi wakati kutakapokuwa na matukio ya ubaguzi wa rangi na kuongeza kuwa “watawaunga mkono” wote watakaofuata ushauri wao. 

Katika maazimio yaliyofikiwa na Chama cha Klabu za Soka za Ulaya (ECA) na Shirikisho la Wachezaji wa Kulipwa Duniani (FIFPro), shirikisho hilo la soka la Ulaya likawakumbusha marefa kuwa wameruhusiwa tokea miaka minne iliyopita kusimamisha mechi kukitokea tukio lolote kubwa la ubaguzi wa rangi jukwaani au uwanjani.

Maazimio hayo pia yamewataka makocha na wachezaji kukemea vitendo vya ubaguzi wa rangi hata kama wakijua kuwa kufanya hivyo kunawakosoa “mashabiki na wachezaji wao wenyewe".

Maazimio hayo yaliandaliwa na Baraza la Mikakati ya Soka (PFSC) na kupitishwa na kamati ya utendaji ya  UEFA, iliyokutana Bulgaria Alhamisi. PFSC inaundwa na wawakilishi kutoka UEFA, ligi za taifa, klabu za Ulaya na wachezaji.

Maazimio yanapendekeza na kuunga mkono uamuzi wa kutaka marefa wasimamishe mechi kukitokea ubaguzi na pia kutaka vyama vya soka na ligi kuu pia kutekeleza maazimio haya".

Mwaka 2009, UEFA ilitaja hatua tatu za kufuata kabla ya kusimamisha mechi.

Iilisema kwamba refa ni lazima kwanza asimamishe mechi na kuomba matangazo yatolewe kwa mashabiki. Hatua ya pili itakuwan ni kuahirisha mechi kwa kipindi fulani na, mwishowe, kuvunja kabisa mechi husika.

Hadi sasa, hakuna mechi yoyote iliyoandaliwa na UEFA iliyowahi kuvunjwa na, licha ya maelekezo hayo, kumekuwa na mechi kadhaa ambazo ziliendelea kuchezwa licha ya uzomeaji wa kibaguzi, likiwamo tukio la hivi karibuni kwenye mechi ya ligi ya Europa kati ya Inter Milan na Tottenham Hotspur.

Kevin-Prince Boateng wa AC Milan alitoka uwanjani kwa hasira baada ya kufanyiwa vitendo vya ubaguzi na mashabiki wakati wa mechi ya kirafiki dhidi ya timu inayoshiriki ligi ya daraja la chini Italia ya Pro Patria Januari na baada ya hapo mechi hiyo ikavunjwa.

Maazimio hayo pia yameitaka UEFA, vyama vya soka vya kitaifa na ligi kuu kutunga kanuni mpya zitakazotoa adhabu kali dhidi ya vitendo vya ubaguzi.

No comments:

Post a Comment