Sunday, January 27, 2013

JERRY TEGETE AENDELEZA MAKALI ALIYOPATA UTURUKI KWA KUTUPIA 2 WAKATI YANGA IKIIDUNGUA PRISONS 3-1


Simon Msuva wa Yanga (kushoto) akimtoka beki wa Prisons wakati wa mechi yao ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo.
STRAIKA Jerry Tegete aliye katika kiwango chake cha juu alifunga magoli mawili na beki wa kimataifa wa Rwanda, Mbuyu Twite akaongeza jingine wakati Yanga wakiibuka na ushindi mnono wa mabao 3-1 dhidi ya ‘maafande’ wa Prisons ya Mbeya na kuendelea kujichimbia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara leo.
 
Tegete aliyerejea katika makali yake na kufunga karibu katika kila mechi anayopangwa tangu Yanga  waliporejea nchini kutoka katika kambi yao ya wiki mbili nchini Uturuki, alifunga goli la utangulizi la timu yake katika dakika ya tisa tu ya mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa na kuhudhuriwa na maelfu ya mashabiki.

Winga Simon Msuva aliyeng’ara na kuonekana kuwa nyota wa mchezo alikimbia na mpira katika upande wa kulia wa uwanja na kupiga krosi ‘kali’ iliyounganishwa moja kwa moja na Tegete na kuwa miongoni mwa magoli bora kuwahi kufungwa na ‘Wanajangwani’ msimu huu.

Dakika tano baadaye, Elias Maguri aliisawazishia Prisons 14 baada ya kuwachambua mabeki wa Yanga ‘kama karanga’ na kuingia ndani ya boksi ambapo pia alimlamba chenga kipa Ali Mustafa ‘Barthez’ kabla ya kuukwamisha mpira wavuni kirahisi kwa kupiga shuti jepesi kuelekea katika lango lililokuwa tupu. 

Maafande waliendelea kucheza ‘jihadi’ na kukaribia kupata goli la utangulizi wakati Jeremiah Juma alipobaki yeye na kipa katika dakika ya mwisho ya kipindi cha kwanza baada ya kupenyezewa pasi safi ya ‘goli’ na Nurdin Siha lakini akashikwa kigugumizi na mwishowe Barthez akauwahi mpira kutoka miguuni mwake. Hadi mapumziko, matokeo yalikuwa sare ya 1-1. 

Prisons walikianza kipindi cha pili kwa kasi zaidi na kulishambulia mfululizo lango la Yanga kiasi cha kuzima shangwe za mashabiki wa ‘Wanajangwani’ waliofunika jukwaa kwa fulana za kijani na njano huku mahasimu wao wa jadi, Simba wakishangilia pasi kali za ‘maafande’ hao wa Mbeya.

Hata hivyo, wenyeji walizinduka na kurejesha furaha kwa mashabiki wao baada ya kupata goli la pili katika dakika ya 57 lililofungwa na Mbuyu Twite kufuatia mpira wa kona ‘kali’ iliyopigwa na Niyonzima kuuanganishwa vyema na Msuva kabla ya kutemwa na kipa Abdallah na kumkuta beki huyo wa kimataifa wa Rwanda aliyeukwamisha wavuni kwa shuti kali la karibu na lango.

Baada ya bao hilo, Yanga waliendelea kucheza gonga safi zilizoonyesha matunda ya maandalizi yao ya wiki mbili nchini Uturuki ambapo katika dakika ya 64, ‘muvu’ iliyomaliziwa kwa krosi ya Nurdin Bakari ilimkuta Tegete katika nafasi nzuri na bila kufanya makosa, mshambuliaji huyo wa zamani wa timu ya taifa (Taifa Stars) akafunga kwa kuudokolea mpira wavuni.

Kocha wa Yanga, Mholanzi Ernst Brandts aliwasifu wapinzani wao na kueleza kuwa amefurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu yake, hasa katika kipindi cha pili. 

Kocha Jumanne Chale wa Prisons alisema kuwa timu yake ilipoteza mechi hiyo kutokana na sababhu za kiufundi, hasa kwa kumkosa mshambuliaji wao Emmanuel Gabriel aliyeondolewa kikosini muda mfupi kabla ya mechi baada ya kibali chake kukosekana.  

Ushindi wa leo umeifanya Yanga izidi kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kufikisha pointi 32, tano zaidi ya Azam wanaokamata nafasi ya pili baada ya kushinda 3-1 dhidi ya Kagera Sugar jana na sita zaidi ya mahasimu wao wa jadi, Simba ambao wamebaki katika nafasi ya tatu licha ya kuibuka na ushindi wa 3-1 pia dhidi ya African Lyon jana.

VIKOSI
Yanga: Ali Mustafa ‘Barthez’, Mbutu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Athumani Iddi ‘Chuji’, Simon Msuva, Nurdin Bakari/David Luhende (dk.59), Didier Kavumbagu/Hamis Kiiza (dk.54), Jerry Tegete na Haruna Niyonzima.  

Prisons: David Abdallah, Aziz Sibo, Henry Mwalugala, Jumanne Fadili, Nurdin Issa, Sino Augustino, Fredy Chudu, Elias Maguri/Julisu Kwanga (74), Misango Magai/John Matei (58) na Jeremiah Juma.


No comments:

Post a Comment