Friday, January 4, 2013

HATUTAMFUKUZA BALOTELLI, TUTAMPA NAFASI NYINGINE 100 ZA KUJIREKEBISHA, ASEMA MANCINI

Mancini (kulia) akimvuta jezi Balotelli
Wafanyakazi wa uwanjani wakiwatenganisha
Balotelli (wa pili kushoto) akiondolewa huku Mancini (kulia) akimbwatukia

Balotelli (kulia) akiondolewa kutoka katika eneo la tukio huku Mancini (kushoto) akishuhudia

 Mancini akionekana katika hali ya fadhaa baada ya tukio lake na Balotelli

 Mancini akionekana katika hali ya fadhaa baada ya tukio lake na Balotelli
Balotelli (kushoto) na Mancini (wa pili kushoto) wakishiriki mazoezi kabla ya tukio baina yao lililozua gumzo.

KOCHA wa Manchester City, Roberto Mancini amesema atampa Mario Balotelli "nafasi nyingine 100 zaidi" za kujirekebisha baada ya kusisitiza kuwa malumbano yake na mshambuliaji huyo hayakuwa ni ngumi.

Picha zinaonyesha wawili hao wakitenganishwa wakati wa mazoezi yao ya jana.

Lakini Mancini alisema kuhusu tukio hilo kwamba kilichotokea na Muitalia mwenzake huyo: "Si ngumi, siyo kweli. Picha zinaelezea vibaya tukio.

"Nitampa nafasi nyingine 100 kama nadhani inawezekana akabadilika. Nampa nafasi nyingine, hakika, kwa sababu ana umri wa miaka 22 na anaweza kufanya makosa."

Tukio hilo hilo jipya zaidi katika mfululizo wa matukio ya utata yanayomhusisha mshambuliaji huyo, limemuonyesha Balotelli katika picha akikunjana na kocha wake.

Picha zinaonyesha Mancini akimbwatukia mchezaji wake huyo, ambaye amefunga magoli matatu katika mechi 21 msimu huu.

Picha moja inawaonyesha wawili hao wakiangaliana uso kwa uso, nyingine Mancini akivuta jezi ya Balotelli, wakati katika picha nyingine mshambuliaji huyo anaonekana akivutwa pembeni na wafanyakazi wa uwanjani hapo.

Lakini Mancini amedai kwamba tukio hilo limekuzwa mno na kusisitiza kwamba Balotelli anahitaji klabuni hapo.

"Haikuwa mbaya," alifafanua. "Tulikuwa tunacheza mechi, Mario akampiga teke mwenzake nikamwambia 'nenda ndani (kwenye vyumba vya kuvalia), ondoka uwanjani'.

"Alisema 'hapana' hivyo nikamvuta shati lake na kumsukuma nje ya uwanja. Hicho ndicho kilichotokea. Hakuna cha zaidi."

"Mario yuko hivi lakini mtazamo wangu (kuhusu hatma yake) hautabadilika, hii siyo muhimu. Tatizo litakuwa yeye mwenyewe. Kama hatabadilika, kwake itakuwa ngumu sana huku baadaye. Kwake, si kwangu.

"Mario anaweza kubaki nami siku moja, mwezi mmoja, miaka mitano. Ana miaka 22. Anahitaji kubadilika. Tatizo lake ni yeye mwenyewe."

Alipoulizwa kama ni yeye ndiye aliyepandisha hasira katika tukio hilo, Mancini alijibu: "Hapana. Kwa sekunde mbili za kwanza, ndiyo, lakini baada ya sekunde tatu ama nne hakutaka kuondoka uwanjani. Kwangu alipaswa kuondoka."

No comments:

Post a Comment