Monday, December 17, 2012

RONALDO ANASTAHILI TUZO YA BALLON D'OR - GULLIT

Cristiano Ronaldo
Ruud Gullit

GWIJI wa soka wa Uholanzi, Ruud Gullit amesema nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo anastahili kushinda tuzo ya Ballon d'Or ya Mwanasoka Bora wa Dunia dhidi ya Lionel Messi wa Barcelona.

Nyota huyo wa zamani wa Chelsea na AC Milan ni mmoja wa washereheshaji wa tuzo za Ballon d’Or mjini Zurich Januari 7.

Gullit alisema: "Ronaldo anastahili kupata tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia.

"Anastahili zaidi kuliko Messi na hastahili kudhalilishwa na FIFA na waandaaji wa tuzo katika chumba ambacho analazimika kwenda kila siku na kushuhudia Messi anavyompiku kwenye tuzo mbele yake.

"Katika tuzo za mwaka jana za UEFA Awards, katika tuzo ya Mwanasoka Bora wa Ulaya, Ronaldo alikosa. Lakini akahudhuria tena na kukaa katika siti ya mbele.

"Namheshimu Cristiano sana kwa kufanya hivyo. Lakini naamini atamwambia kila mtu kwamba hatahudhuria tena tuzo hizo kama mambo yataendelea kuwa mabaya kwake tena."

Gullit, ambaye alishinda tuzo ya mwanasoka bora wa dunia mara mbili, aliendelea: "Cristiano anastahili kuthibitishwa kwamba yeye ni mchezaji mzuri sana. Wanaweza kufanya jambo hilo kwa kumpa tuzo ya Ballon d’Or. Na kwangu mimi yeye ndiye mchezaji bora wa mwaka 2012. Nataka sana tuzo hii kubwa binafsi ya soka iende kwake.

"Yeye ni mchezaji mkali ambaye ana ubora ambao kila mchezaji wa kiwango cha juu anauhitaji.

"Ana mwili mkubwa, ni ngangari, anapiga vichwa vizuri, anaweza kumiliki mpira, ana kasi, anapiga 'fri-kiki' za hatari na ­penalti. Na anaweza kushuti golini kutokea pande zote. Na zaidi ya hayo anajipanga vizuri sana kiufundi.

"Pamoja na Messi yuko katika kategori ya watu 'spesho'. Hakika, Messi alivunja rekodi maarufu ya Gerd Muller ya magoli 85 ndani ya mwaka mmoja wiki iliyopita.

"Rekodi hiyo bila ya shaka itambeba Messi katika upigaji kura. Lakini katika macho yangu Ronaldo yuko vizuri sana.

"Cristiano daima anaishia kuwa wa pili. Lakini anastahili kuwa wa kwanza kama Messi.

"Wanapaswa wamualike mshindi tu kwenye tuzo na wamuepushie namba mbili kudhalilika."

No comments:

Post a Comment