Monday, December 10, 2012

PACQUIAO ADUNDWA KWA KO LICHA YA KUMVUNJA PUA MPINZANI WAKE… AHATARISHA PAMBANO LAKE LA SH. BILIONI 300 DHIDI YA FLOYD MAYWEATHER…!


Shoka moja mbuyu chini...! Pacquiao akiangukia uso baada ya kutandikwa ngumi kali katika raundi ya sita na kutwangwa kwa KO dhidi ya Marquez katika pambano lao mjini Las Vegas, Marekani usiku wa kuamkia jana Desemba 8, 2012. 
Inuka sasa....! Pacquiao akimuangalia mpinzani wake Marquez baada ya kumpeleka sakjafuni katika raundi ya tano.
Chaliiii....! Pacquiao akiwa sakafuni
Weweeeeee.....! Marquez akishangilia baada ya kumchapa Pacquiao kwa KO usiku wa kuamkia jana..
Mmmhh... nimeshinda lakini chamoto nimekiona...! Marquez anavyoonekana usoni baada ya kutandikwa ngumi zaidi ya 90 na Pacquiao usiku wa kuamkia jana Desemba 8, 2012.
LAS VEGAS, Marekani
Pambano linalofukuziwa na Manny Pacquiao dhidi ya Floyd Mayweather, likiwa na thamani ya takriban dola za Marekani milioni 200 (Sh. bilioni 300), liliangukia sakafuni mjini Las Vegas wakati Mfilipino huyo alipopigwa ‘kiajabu’ kwa KO katika raundi ya sita na raia wa Mexico, Juan Manuel Márquez.

Pacquiao alisema baada ya kumalizika kwa pambano hilo kuwa hatastaafu lakini kipigo hicho kimempunguzia nguvu promota wake Bob Arum katika mazungumzo kuhusu mgawo wa pambano wanalolifukuzia kwa udi na uvumba dhidi ya Mayweather.

Majadiliano kuhusu pambano la Pacquiao na Mmarekani Mayweather ambaye hajawahi kupigwa yamekwama mara kadhaa katika kipindi cha miaka mitatu sasa.

Pambano alilopigwa Pacquiao linaweza kuitwa kuwa “pambano la mwaka” baada ya wababe hao kuchapana vikali kwa namna ya kusisimua. 

Wakiwa wamechuana vikali katika kila mapambano yao matatu yaliyotangulia, ambayo Pacquiao alishinda mawili kwa tofauti ya pointi chache na kuzua utata kuwa alibebwa huku jingine likimalizika kwa sare, wote wawili waliapa kuonyesha kiwango cha juu ili kumaliza ubishi kati yao. Na kweli, walionyesha kiwango cha juu mno kama wenyewe walivyoahidi.

Pacquiao alipelekwa sakafuni katika raundi ya tatu lakini baadaye akajibu mapigo kwa kumpeleka chini Márquez katika raundi ya tano.

Wawili waliendelea kuchapana vikali hadi katika raundi ya sita wakati Pacquiao alipotwangwa ngumi kali na kuanguka vibaya, akitanguliza uso juu ya sakafu kabla ya mwili kufuata.

Refa Kenny Bayless, alipunga mikono hewani kuahsiria mwisho wa pambano hilo wakati Márquez akishangilia na kuibua shangwe kutoka kwa mashabiki wake ndani ya ukumbi wa MGM.

Pacquiao alibaki sakafuni kwa takriban dakika mbili kabla wapambe wake hawajamsaidia kusimama.

“Nilirusha ngumi jiwe,” Márquez alisema.
“Nilijua Manny atanipiga kwa KO katika dakika yoyote ile. Nilifikiri kwamba atanipiga kwa KO katika raundi tatu za mwisho na nilijua kwamba ataachia nafasi.”

Licha ya ushindi wake, Marquez chamoto alikiona kwani alipigwa ngumi 94 zilizompata kisawasawa dhidi ya 52 alizorusha yeye. Márquez pia alishavunjwa mfupa wa pua kabla ya raundi ya sita na muda wote alikuwa akivuja damu na kupumua kwa shida.

Hadi kufikia raundi ya tano, majaji wote walikuwa wakimpa Pacquiao ushindi wa pointi 47–46.

“Nimepigwa kwa ngumi ambayo sikuiona,” alisema Pacquiao baada ya pambano hilo, huku akipepesa macho yake kwa shida.

Kabla ya pambano la usiku wa jana, Pacquiao ambaye pia ni msanii wa muziki na mwanasiasa maarufu anayeshikilia ubunge katika jimbo moja nchini kwao (Phillipines), alikuwa hajawahi kupigwa kwa KO tangu mwaka 1999.

No comments:

Post a Comment