Thursday, December 20, 2012

KIMENUKA POLISI....! SASA WAANZA KUCHUNGUZANA KUHUSU NANI KATI YAO ALIYETIA KIBINDONI SH. MILIONI 150 ZILIZOPORWA NA MAJAMBAZI KARIAKOO JIJINI DAR ES SALAAM JUZI.... TIMU YA UCHUNGUZI INAONGOZWA NA POLISI WENYEWE CHINI YA WASAIDIZI WATANO WA KAMANDA KOVA AKIWAMO MKUU WA UPELELEZI KANDA MAALUM YA DAR ES SALAAM, AHMED MSANGI... NI BAADA YA KUFICHULIWA KWA TAARIFA KUWA BAADHI YAO WALIPORA MIHELA HIYO KUTOKA KWA MAJAMBAZI NA KUGAWANA WENYEWE BILA AIBU!

Kamanda Kova
Baadhi ya Polisi wakiwa kazini katika siku ya tukio hilo la ujambazi wa Sh. milioni 150, eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam, juzi Desemba 18, 2012.  
Mmoja wa watuhumiwa wa tukio la ujambazi wa Sh. milioni 150 uliofanyika Kariakoo jijini Dar es Salaam juzi Desemba 18, 2012 aitwaye Augustino akiwa chini ya ulinzi wa vijana wa Kamanda Kova. 

Jeshi la Polisi katika Kanda Maalum ya Dar es Salaam limeunda timu yake maalum ya uchunguzi kubaini ukweli kuhusu madai kwamba baadhi ya polisi walipora 'fuko' la fedha lililokuwa na Sh. milioni 150 zilizoporwa katika duka la matairi na spea za magari eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam na kugawana wenyewe zote badala ya kuziwasilisha kituoni, imefahamika.

Akizungumza leo mchana (Desemba 20, 2012), Kamanda wa Polisi katika kanda hiyo, Suleiman Kova, amesema kuwa timu yenye maafisa watano wa juu wa polisi itafanya kazi hiyo ndani ya siku saba, huku ikiongozwa na Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Ahmed Msangi.

Kamanda Kova alisema kuwa wao ni wazoefu, na hivyo anaamini kuwa ndani ya siku saba tu, watakuwa tayari wamepata ukweli wa kila kitu kuhusiana na tuhuma hizo na kwamba, wahusika wote watajulikana na kuchukuliwa hatua zinazostahili ikiwa madai hayo ni ya kweli.

Kova akawaomba wananchi wote kutoa ushirikiano kwa kufikisha taarifa zote muhimu zitakazosaidia kupatikana kwa askari wanaodaiwa kugawana fedha hizo zinazodaiwa kukwapuliwa kutoka kwa majambazi; ambao nao waliwaua watu wawili kwa risasi na kuwajeruhi wengine kadhaa wakati wakizipora kutoka katika duka la matairi kwenye maeneo ya Mtaa wa Mchikichini, Kariakoo jijini Dar es Salaam.

Leo, baadhi ya vyombo vya habari, likiwamo gazeti la Uhuru linalomilikiwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) ziliwakariri baadhi ya mashuhuda wa tukio la ujambazi wa Kariakoo waliosema kuwa walishuhudia polisi wakibeba 'fuko' hilo la fedha baada ya kulitwaa kutoka kwa majambazi na kwenda kugawana; huku wengine wakisema kuwa 'mchongo' huo ulifanikishwa katika maeneo ya Jangwani.

Watuhumiwa watatu wa ujambazi huo uliotokea juzi walitiwa mikononi mwa polisi, akiwamo mmoja aliyetajwa kwa jina la Augustiono.

No comments:

Post a Comment