Wednesday, December 26, 2012

KABANGE TWITE AANZA VIBAYA… YANGA YACHEZEA KICHAPO KWA TUSKER

George Banda wa Yanga (kulia) akijaribu kuwatoka mabeki wa Tusker leo Desemba 26, 2012. 

Yanga iliwasononesha mashabiki wake katika siku ya kukamilisha sherehe za sikukuu ya krismasi (boxing day) baada ya kubanwa kwa muda mwingi na kukubali kipigo cha bao 1-0 katika mechi yao ya kirafiki dhidi ya Tusker ya Kenya kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam jana.
Wageni walifanya mashambulizi mengi na kutangulia kupata goli walilostahili kwa njia ya penati katika dakika ya mwisho ya kipindi cha kwanza baada ya Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kumuangusha Khalid Aucho wa Tusker ndani ya ‘boksi’ na refa Israel Nkongo kuamuru penati iliyowekwa wavuni kiufundi na Ismail Dunga.
Mashabiki wa Yanga walikuwa na wakati mgumu kutokana na mashambulizi mengi zaidi kuelekea langoni mwao, lakini kipa kipa Ali Mustafa ‘Barthez” alifanya kazi kubwa ya kupunguza idadi ya mabao kwa kuokoa michomo kadhaa ya hatari.
Kocha wa Yanga, Mholanzi Ernie Brandts alisema baada ya mechi hiyo kuwa hakushangazwa na kipigo hicho kwani nyota wake kadhaa wa kikosi cha kwanza hawakucheza, wakiwamo Mbuyu Twite, Kelvin Yondani, Haruna Niyinzima ‘Fabregas’ na kinara wa mabao katika mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Didier Kavumbagu,
Hata hivyo, Kabange Twite ambaye ni  pacha wa Mbuyu Twite aliyetua Yanga katika kipindi cha usajili wa dirisha dogo alionyesha kiwango cha juu na kushangiliwa kila mara kutokana na uchezaji wake wa ‘jihadi’ kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mechi.
Miongoni mwa nafasi chache walizopoteza Yanga ni pamoja na dakika ya pili tu iliyopotezwa na George Banda,  ‘tik-taka’ ya Said Bahanunzi iliyoparaza kidogo ‘besela’ katika dakika ya 43 na kichwa cha Cannavaro kilichookolewa na kipa Samwel; Odhiambo katika dakika ya 83.
Tusker walipoteza nafasi nyingi za kuongeza mabao pia, zikiwamo za dakika ya sita na 34 kupitia kwa Dunga na dakika ya 86 wakati Edru Sekayonga alipobaki na Barthez lakini akapiga shuti lililombabua usoni kipa huyo na kumuumiza kiasi cha kufanya mechi isimame kwa dakika mbili ili atibiwe.
Kipigo cha jana ni cha pili kwa Yanga katika mechi 10 tangu Brandts aanze kuiongoza baada ya kurithi mikoba ya kocha aliyetimuliwa, Mbelgiji Tom Saintfiet.
 Hii ilikuwa ni mechi ya pili Tusker ambao ni mabingwa wa Kenya, watateremka tena dimbani mwishoni mwa wiki kucheza dhidi ya mabingwa wa Tanzania, Simba. 
Vikosi:
Yanga:
Ally Mustapha ‘Barthez’, Juma Abdul, Oscar Joshua/Simon Msuva, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Ladislaus Mbogo/Stephano Mwasika, Nurdin Bakar, Rehan Kibingu/Omega Seme, Kabange Twite, Said Bahanunzi, George Banda/Hamis Kiiza, David Luhende.

Tusker:
Samwel Odhiambo, Luke Ochiend, Jeremial Bright, Mark Odhiambo, Joseph Shikokoti, Khalid Aucho, Edwin Manono, Justine Monda, Ismail Dunga/Edru Sekayonga (dk.46), Jesse Were/Andrew Tololwa, Robert Omonuki.

No comments:

Post a Comment