Thursday, December 27, 2012

ROONEY NJE WIKI TATU

Wayne Rooney

Wayne Rooney


WAYNE Rooney huenda akawa nje ya uwanja kwa wiki tatu baada ya kuumia goti.

Straika huyo wa Manchester United (27) huenda akakosa mechi nne, ikiwamo ya Kombe la FA dhidi ya West Ham.

"Wayne alijaribu kupiga mpira wa mkunjo wa ndizi mazoezini na akaumia goti - atakuwa nje kwa wiki mbili ama tatu," kocha wa Man United, Sir Alex Ferguson aliiambia BBC Sport.

Rooney, ambaye amefunga magoli saba katika ligi msimu huu, alipumzishwa na nafasi yake ikachukuliwa na Javier Hernandez 'Chicharito' katika ushindi wa Man U wa 4-3 dhidi ya Newcastle.

Alicheza kwa kiwango kibovu dhidi ya Swansea wikiendi na Ferguson alitarajia angerejea vyema katika mechi dhidi ya Newcastle.

"Baada ya kiwango chake cha Jumapili nilidhani angecheza vizuri leo. Huwezi kucheza mechi mbili kwa kiwango kama kila cha Jumapili," aliongeza Mscotland huyo, ambaye atatimiza umri wa miaka 71 kuamkia Mwaka Mpya. "Lakini hatukuweza kumhatarishia."

Kama Rooney atakosa kipindi chote hicho atakosa mechi dhidi ya West Brom Jumamosi, Wigan siku ya Mwaka Mpya, mechi ya Kombe la FA dhidi ya West Ham Januari 5 na ya upinzani wa jadi dhidi ya mahasimu Liverpool Januari 13.

Alikuwa nje kwa mwezi mzima mapema msimu huu baada ya kuumia mguu wa kulia.

Aidha, straika Danny Welbeck na winga Ashley Young pia walikosa mechi ya Boxing Day kwenye Uwanja wa Old Trafford.

"Welbeck aliugua katika hoteli ya timu jana (juzi) usiku," Ferguson alisema. "Ashley Young pia aliumia jana (juzi) na Phil Jones aliumia dhidi ya Swansea.

"Young anatarajiwa kurejea Jumamosi (dhidi ya West Brom)."

Ferguson alifafanua sababu ya kumuacha benchi nahodha Nemanja Vidic dhidi ya Newcastle siku chache baada ya kuanza kwa mara ya kwanza msimu huu katika kikosi cha kwanza dhidi ya Swansea.

"Huwezi kumhatarishia Vida baada ya kucheza mechi yake ya kwanza," alisema.

"Alikuwa na uzito katika goti lake, ambao ulitarajiwa baada ya kuwa nje kwa muda mrefu sana."

Manchester United wamepata pointi 46 msimu huu hadi sasa, lakini zaidi ya nusu ya hizo (24) wamezipata katika mechi ambazo walitanguliwa angalau mara moja.

No comments:

Post a Comment