Tuesday, November 6, 2012

PETER ODEMWINGIE ATUPIA MAWILI WAKATI WEST BROM WAKISHINDA 2-0 NA KUPANDA HADI KATIKA NAFASI YA TANO KWENYE MSIMAMO WA LIGI KUU YA ENGLAND




Natishaaa...!  Peter Odemwingie akishangilia goli alilofunga dhidi ya Southampton wakati wa mechi yao ya Ligi Kuu ya England mjini West Bromwich, jana Novemba 5, 2012.

Peter Odemwingie wa West Bromwich Albion (kulia) akifunga goli dhidi ya Southampton wakati wa mechi yao ya Ligi Kuu ya England mjini West Bromwich, jana Novemba 5, 2012.
LONDON, England
PETER Odemwingie alifunga mara mbili kuisaidia West Bromwich Albion kuendeleza mwanzo wao mzuri msimu huu kwa ushindi wa 2-0 dhidi ya timu inayoburuta mkia ya Southampton na kukwea hadi katika nafasi ya tano kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England jana.

Shuti la mshambuliaji Odemwingie katika dakika ya 36 lilifungua akaunti ya magoli ya wenyeji na Mnigeria huyo akaongeza jingine katika dakika ya 60 baada ya kuunganisha vyema kwa kichwa cha karibu na lango krosi ‘kali’ ya Shane Long.

West Brom wana pointi 17 kutokana na mechi 10, sawa na timu inayokamata nafasi ya nne ya Everton na saba nyuma ya vinara Manchester United.

Southampton wamejikusanyia pointi nne, sawa na Queens Park Rangers ambayo haijawahi kushinda, lakini wako mkiani mwa msimamo wa ligi kutokana na tofauti ya mabao.

West Brom wamepoteza pointi katiika mechi zao mbili zilizopita dhidi ya mabingwa Manchester City na pia Newcastle United, kwa kuruhusu magoli ya dakika za majeruhi lakini safari hii hawakufanya makosa dhidi ya kikosi cha Southampton.

Zoltan Gera alipoteza nafasi ya wazi katika dakika ya 20 wakati shuti la Odemwingie lilipokwenda moja kwa moja miguuni mwake lakini akiwa umbali wa yadi sita kutoka golini akapiga shuti lililopaa juu ya lango.

Baada ya goli la utangulizi la Odemwingie lililotokana na shuti lililomparaza Maya Yoshida na kumpita kipa Paulo Gazzaniga, Southampton walikosa bahati ya kusawazisha baada ya shuti la Rickie Lambert kugonga ‘besela’ mwanzoni mwa kipindi cha pili.

Kipa wa West Brom, Ben Foster alifanya kazi nzuri ya kuokoa na kuinyima Southampton goli katika muda wa majeruhi.

Odemwingie alifurahishwa na kiwango cha timu yake baada ya kupata vipigo katika dakika za majeruhi kutoka kwa Man City na Newcastle.

"Haya yalikuwa majibu mazuri kutoka kwa timu nzuri. Tulihitaji bahati kidogo na ni rahisi, kama mkiendelea kupiga mashuti mtafunga, tumefurahi kupata pointi zote tatu," Odemwingie aliiambia Sky Sports.

No comments:

Post a Comment