Wednesday, November 21, 2012

MESSI ABAKISHA REKODI YA RAUL TU ULAYA

Lionel Messi a.k.a "Jini" a.k.a "Genius"
Messi akifunga goli dhidi ya Spartak Moscow jana usiku. Barca ilishinda 3-0.


LIONEL Messi anaendelea kuvunja rekodi moja baada ya nyingine. Mjini Moscow jana usiku alikuwa akiifukuzia rekodi ya Ruud Van Nistlerooy na akaifikia. Muargentina huyo haachi kitu na kidogo kidogo anazipangua rekodi zilizo mbele yake.

Kwa magoli yake mawili aliyofunga kwenye uwanja wa Luzhniki dhidi ya Spartak Moscow jana, amefikisha juma la mabao 56 katika michuano ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya, sawa na magoli yaliyofungwa na mshambuliaji wa zamani wa klabu za PSV, Manchester United na Real Madrid, Van Nistelrooy.

Messi hivi sasa ni wa pili katika orodha ya vinara wa mabao mengi katika michuano hiyo, akiwa amepitwa na Raul Gonzalez tu.

Mchezaji huyo wa zamani wa Real Madrid alifunga magoli 71 katika michuano hiyo.

Lakini kutokana na kasi aliyonayo Messi huku akiwa ndiyo kwanza ana umri wa miaka 25, rekodi ya Raul iko matatani sana kwani bado magoli 15 tu kumfikia.

Messi jana pia alifikia rekodi nyingine. Magoli yake mawili yamemfanya kufikia rekodi ya Vivian Woodward ambaye, mwaka 1909, alifunga magoli 25 katika mechi za kimataifa za klabu yake na timu ya taifa katika mwaka mmoja.

Pamoja na hayo, magoli aliyofunga yamemfanya Urusi yamemfanya Muargentina huyo kuwa amefunga magoli katika nchi zote 14 alizoenda kucheza soka kwani nchi hiyo ndiyo ilikuwa ardhi pekee aliyokuwa bado hajatupia goli.

Magoli hayo mawili ya Messi, pia yanamaanisha kwamba sasa amebakisha magoli matano tu kumfikia Gerd Muller ambaye anashikilia rekodi ya muda wote ya kufunga magoli mengi zaidi katika mwaka mmoja akiwa na magoli 85.

Messi ana mechi tisa za kuipita rekodi hiyo: moja ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya, tano za La Liga na tatu za Kombe la Mfalme, kama Barca itaitoa katika michuano hiyo Alaves katika mechi yao ya marudiano wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment