Friday, October 26, 2012

MTAZAME MTOTO WA KIBRAZIL ASIYE NA MAKANYAGIO ANAYEMZIMIA MESSI ALIPOKUTANA NA SHUJAA WAKE NA KUMSHANGAZA... AJIONA KAMA AMETWAA TUZO YA BALLON D'OR

Ayaaa.. umenipiga tobo.......! Mtoto Gabriel (kushoto) akimpiga chenga shujaa wake Lionel Messi wakati alipopata mwaliko wa kutembelea kambi ya Barcelona 
Mtoto Gabriel akipiga danadana mbele ya shujaa wake Messi (hayupo pichani)
Daah! Dogo we mkali....kula tano! Lionel Messi akimpa 'gwara' mtoto Gabriel baada ya mtoto huyo kuonyesha ufundi wake wa kuchezea mpira
Lazima niache chata... Lionel Messi akisaini jezi ya mtoto Gabriel baada ya kumshangaza kwa kipaji alichonacho cha kuuchezea mpira licha ya kutokuwa na makanyagio


Ngoja nikuguse... umewezaje? We mkali bhana....Dani Alves akichonga na Mbrazil mwenzake, mtoto Gabriel alipowatembelea mazoezini
Beki Eric Abidal (kushoto) anayeendelea kupona kutokana na upasuaji wa kupandikizwa ini aliofanyiwa, pamoja na beki Mbrazil Adriano wakichekeshwa na mtoto Gabriel wakati mtoto huyo alipowatembelea Barcelona mazoezini 

Wewe ni supastaa wa dunia, hebu tupige picha nawe..... Wachezaji wa Barcelona kutoka kushoto kipa Victor Valdes, beki Adriano na Dani Alves wakipozi na mtoto Gabriel (wa pili kulia) wakati alipowatembelea mazoezini

GABRIEL Muniz ni mtoto wa Kibrazil mwenye umri wa miaka 11 ambaye alikuwa na ndoto za kukutana na Lionel Messi siku moja. Na ndoto yake hatimaye imetimia, hasa baada ya habari yake kuwa maarufu na kuwagusa wengi mioyoni huku pia ikiwapa changamoto ya kutokata tamaa ya maisha.

Gabriel hana makanyagio. Alizaliwa hivyo hivyo. Ingawa familia yake ilidhani kwamba angekuwa na matatizo makubwa katika maisha yake ya kawaida, alianza kutembea kabla hajatimiza umri wa mwaka mmoja. Ilimchukua muda mrefu kuweza kuruka kutoka kutembea hadi kucheza mpira, lakini aliweza yote hayo. Na, hakika, hakuna anachopenda zaidi ya kucheza soka.

Anacheza bila ya viatu, na hutumia vifaa maalum kuvaa chini inaponyesha mvua ili kumuepushia kuteleza. Ukimuangalia anavyocheza mpira utashangaa. Ana kasi na "maujuzi" – ana kipaji sana na anafanya kila awezalo kumuiga shujaa wake, Leo Messi.

Gabriel alikuwa na bahati sana kualikwa katika wakati wa mazoezi ya Barcelona, na mwishoni mwa mazoezi akapata fursa ya kukutana na wachezaji, na kuzungumza nao hasa Wabrazil wenzake Dani Alves na Adriano.

Lakini tukio lake kubwa zaidi lilikuwa halijawadia. Pale kocha Tito Vilanova alipomuuliza kama amepata fursa ya kukutana na wachezaji wote, Gabriel alijibu: "Sijaonana na Messi bado".

Hatimaye 'mchawi' huyo wa Kiargentina akatokea. Wote wakaanza kuuchezea mpira na Messi akapigwa na butwaa pale alipoona ufundi wa kuchezea mpira alionao Mbrazil huyo mdogo.

Ilionekana kama ni jambo lisilowezekana kwa mtoto asiye na makanyagio kukimbia na kukokota mpira, achilia mbali kupiga 'vibaiskeli', matobo na tikitaka, lakini yeye anaweza.

No comments:

Post a Comment