Friday, September 14, 2012

LIGI KUU YA VODACOM TZ BARA YAANZA KESHO

Straika wa Simba, Mghana Daniel Akuffor (wa pili kushoto) akijaribu kumpita beki wa Azam, Aggrey Morris (aliyelala chini kuokoa) huku kipa Deogratius Munishi 'Dida' (kulia) akiwa tayari kusaidia wakati wa mechi yao ya Ngao ya Jamii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Jumanne. Simba ilishinda 3-2 na kutwaa ngao katika mechi hiyo ya ufunguzi wa msimu mpya wa LIgi Kuu ya Vodacom itakayoanza kesho.

MICHUANO ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara 2012/2013 inaanza kutimua vumbi kesho (Septemba 15 mwaka huu) ambapo timu zote 14 zitakuwa kwenye viwanja saba tofauti.

Mabingwa watetezi Simba wataikaribisha African Lyon kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mjini Morogoro, Polisi Dodoma watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri wakati jijini Tanga, Mgambo JKT ambayo imepanda daraja msimu huu itaumana na Coastal Union kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

Tanzania Prisons ambayo nayo imerejea VPL msimu huu itaialika Yanga kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya. JKT Ruvu na Ruvu Shooting zitapambana kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam huku Azam ikiwatembelea Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Katiba.

Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans dhidi ya Oljoro JKT. Mechi zote zitaanza saa 10.30 jioni.

Afisa habari wa TFF, Boniface Wambura, amesema jijini Dar es Salaam leo kuwa viingilio katika mechi ya Simba na African Lyon vitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani na bluu, sh. 8,000 viti vya rangi ya chungwa, sh. 15,000 viti vya VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh. 20,000. Viingilio kwa mechi nyingine vitakuwa sh. 3,000 na sh. 10,000.

 

No comments:

Post a Comment