Tuesday, September 18, 2012

KESI YA LULU, JAJI AWAHOJI MAWAKILI MMEILETA KESI HII MAHAKAMA YA RUFANI ILI IWEJE?

Alizabeth Michael "Lulu"
MAPITIO ya maombi ya utata wa umri wa msanii wa filamu Elizabeth Michael maarufu kama Lulu (18), anayekabiliwa na shtaka la mauaji ya msanii mwenzake Steven Kanumba (28), jana yalichukua sura mpya baada ya jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani Tanzania kuhoji mawakili wa pande zote kwanini wamelifikisha suala hilo mahakama hapo badala ya kusubiri usikilizwaji wa awali.

Jopo la majaji watatu liliketi jana wakiongozwa na Mwenyekiti Jaji,  January Msoffe, Bernard Luanda na Edward Rutakangwa saa 3:00 walianza kuuhoji upande wa Jamhuri kwa sababu gani wameomba mahakama hiyo ifanye mapitio.


Upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi  Faraja Nchimbi akisaidiana na Wakili wa Serikali Shadrack Kimaro,  ulidai kuwa umeomba mapitio kwa sababu uamuzi uliotolewa na Jaji Dr. Fauz Twaib alikiri maombi ya utetezi hayakuwasilishwa mahakamani kihalali kwa mujibu wa sheria.


Alidai kuwa, Jaji Dk. Twaib alitakiwa kuyaondoa  maombi hayo lakini badala yake alikubali kuyasikiliza ilhali alibaini kuwa hayako sahihi.


“Jaji Dk. Twaib alikosea kutoa tafsiri ya kifungu cha 44 (1) cha sheria ya mahakimu alipaswa kutoa maelekezo kwa mahakama ya Kisutu kulingana na makosa aliyoyaona katika uamuzi wa Hakimu Mkazi Augustina Mmbando na siyo kuyasikiliza yeye mwenyewe… tumeamua kuomba mapitio ili yasikilizwe haraka badala ya kukata rufaa,” alidai Nchimbi.


Alifafanua kwamba msingi wa malalamiko yao mahakamani hapo ni kuhusu uamuzi uliotolewa na Jaji Dk. Twaib ulikuwa na dosari kwa kuzingatia bado hoja ya msingi ilikuwa pembeni.


Jaji Msofe aliuhoji upande wa utetezi kwanini shauri hilo limefika Mahakama Kuu Tanzania, wakati Mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji na kwa sababu gani wasingesubiri shauri lianze kusikilizwa katika usikilizwaji wa awali mahakama kuu baada ya upelelezi kukamilika.


Akijibu hoja hizo, wakili wa utetezi Peter Kibatala alidai kuwa  waliwasilisha maombi yao kwa sababu ya kulinda maslahi ya mtoto (mshtakiwa).


Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya jopo la majaji na wakili Kibatala;


Jaji Msofe: Kwanini mmelizungusha kote huku suala la umri wakati lingeweza kutazamwa katika usikilizwaji wa awali utakapoanza mahakama kuu au mngeweza kuipa nafasi kesi ikaendelea kule Mahakama ya Kisutu ambako ingekuwa imeshapiga hatua mbele sasa lakini kama mnapoteza muda kutaka utata wa umri usikilizwe ili iweje?


Kibatala: Watukufu Majaji, lengo letu ni kulinda maslahi ya mtoto (mshtakiwa) hii ni kesi ya mauaji ni lazima kuwe na namna ya kuweka kumbukumbu wakati wa ushahidi wake.


Jaji Msofe: Najisikia vibaya leo hii kukaona katoto kamekaa pale kizimbani. Huu ubishi wa kesi hii ya mauaji inayomkabili mshtakiwa, kuhusu umri ili iweje?


Kibatala: Hatukuwa na namna ya kuingiza ushahidi wa umri isipokuwa kwa kuomba mahakama ichunguze umri ili itakapofikia usikilizwaji wa kesi ya msingi iweze kuwa na kumbukumbu sahihi.


Jaji Luanda: Huyu sio mtoto wa kwanza kushtakiwa kwa kesi ya mauaji. Kifungu cha 26 cha kanuni ya adhabu lazima kiangalie adhabu ya mtoto anayekabiliwa na kesi kama hii labda mngeweza kutuambia kwamba Lulu hawezi kushtakiwa mnatuambia umri wake  ili iweje?


Kibatala: Tutaondoa shauri kwa ajili ya kurejesha Mahakama ya Kisutu ili kuendelea na usikilizwaji wa awali kabla upelelezi haujakamilika na kuhamishiwa Mahakama Kuu kwa ajili ya usikilizwaji wa kesi ya msingi.


Mwenyekiti wa jopo hilo, Jaji Msofe alisema watakwenda kutafakari hoja zilizotolewa na pande zote mbili ambapo watazijulisha pande hizo tarehe ya hukumu kama kesi hiyo iendelee kusikilizwa utata wa umri Mahakama Kuu ama jalada lirejeshwe Mahakama ya Kisutu kwa ajili ya usikilizwaji wa awali.


Mbali na Wakili Kibatala, mawakili wengine wa utetezi ni Kennedy Fungamtama na Fuljence Massawe ambapo waliwasilisha maombi mahakama kuu wakidai kuwa Lulu ana umri wa miaka (17) na siyo miaka (18) kama ilivyoandikwa kwenye hati ya mashtaka.


Katika kesi hiyo, Lulu anadaiwa kuwa  Aprili 7, mwaka Sinza Vatican, jijini Dar es Salaam, mshtakiwa alimuua Kanumba.


Aidha, kwa mujibu wa Mwenendo wa Sheria ya Makosa ya Jinai (CPA), Lulu hakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji lakini mara upelelezi wake utakapokamilika itahamishiwa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment