Tuesday, September 25, 2012

FIFA KUISHUSHA DARAJA YANGA, PAPIC ASHITAKI AKIDAI MAMILIONI

Kocha wa zamani wa Yanga, Kostadin Papic

KOCHA wa zamani wa Yanga, Mserbia Kostadin Papic amewasilisha FIFA mashitaka yake ya madai ya dola 12,300 (zaidi ya Sh. milioni 15) zinazotokana na malimbikizo ya mshahara wake wakati akiifundisha klabu hiyo.

Kwa mujibu wa barua iliyoifikia TFF kutoka kwa FIFA, Papic alikuwa akiwasiliana na maofisa na viongozi waYanga, lakini hakupata ushirikiano na hivyo kuamua kwenda FIFA.

Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, amesema jijini Dar es Salaam leo kwamba baada ya kupata barua hiyo kutoka FIFA, TFF ilifanya juhudi za kuwasiliana na Yanga kuhusu malalamiko hayo ili kujaribu kumzuia kocha huyo asishtaki FIFA, lakini juhudi hizo hazikuzaa matunda.

"Kama chombo kinachosimamia uendeshaji wa mpira wa miguu nchini, TFF imesikitishwa na habari hizo na inaiomba klabu ya Yanga kufanya kila jitihada kuhakikisha kuwa inawasilisha taarifa zote muhimu na nyaraka zinazohusiana na stahiki za kocha huyo ili kama ilishamalizana naye, sifa ya klabu ya Yanga isafishwe. Tayari barua imeshaandikwa kwa klabu ya Yanga kuitaka itekeleze utashi huo mapemz iwezekanavyo," alisema Osiah.

"Tukio hilo, si tu linachafua sifa ya klabu ya Yanga, bali soka ya Tanzania kwa ujumla kutokana na ukweli kwamba ikishadhihirika kuwa kuna tatizo la malipo ya makocha nchini, ni dhahiri kuwa itakuwa ni vigumu kwa klabu zetu na hata timu za taifa kupata makocha wazuri kutoka nje kwa kuwa watakuwa wamejengeka hofu ya kufanya kazi nchini," aliongeza.

Hili ni tukio la pili kwa Yanga baada ya mchezaji wake mwingine, John Njoroge kuishtaki klabu hiyo FIFA na kushinda kesi yake iliyoamuliwa mwezi Januari na Kitengo cha Usuluhishi wa Migogoro cha FIFA (DRC). Ushindi wa Njoroge unamaanisha kuwa iwapo Yanga itashindwa kutekeleza kumlipa mchezaji huyo kasi cha Sh milioni 17, inaweza kujikuta katika adhabu ambayo itailazimisha TFF iishushe daraja; kuinyang’anya pointi kwa kiwango kitakachotajwa na FIFA; kuipiga faini au adhabu zote kwenda kwa pamoja.

"Tunaiomba Yanga itekeleze hukumu hiyo kwa wakati uliotajwa kwenye barua ya FIFA ili kuepuka hatua hizo," alisema Osiah.

Alisema suala la Njoroge ni moja kati ya matukio mengi yanayohusu ukiukwaji wa taratibu za kuvunja mikataba yanayofanywa na klabu za Tanzania.

"Kuna malalamiko ya wachezaji wengi dhidi ya klabu zao za zamani kuhusu kutolipwa stahiki zao. Hivyo TFF inatoa wito kwa klabu kujiepusha na vitendo hivyo kwa kuwa vinawanyima haki wachezaji, lakini pia vinachafua sifa ya nchi iwapo wachezaji wanachukua hatua za kwenda kwenye vyombo vya juu," alisema.

"Tumekuwa tukisoma kwenye vyombo vya habari kuhusu kutimuliwa kwa sekretarieti nzima ya Yanga kutokana na kuonekana kuwa ina udhaifu. Taarifa hizo hazijaifikia rasmi TFF. Kiutaratibu, Yanga inatakiwa iwaasilishe majina ya maofisa watakaofanya kazi na TFF kwa sasa na itakapoajiri sekretarieti ya kudumu, basi itume barua nyingine ya kuwatambulisha watendaji wake," aliongeza.

Alisema kama Yanga itakuwa imeitimua sekretarieti nzima, basi TFF inapokea taarifa hizo kwa masikitiko makubwa na licha ya kwamba si nia ya TFF kutetea watendaji wazembe, lakini klabu hazina budi kufuatilia kwa karibu utendaji wa sekretarieti zao ili isije ikafikia wakati sekretarieti nzima inaondolewa kwa makosa ambayo yangeweza kusahihishwa kama kungekuwa na ufuatiliaji wa karibu.

Aliongeza kuwa TFF imekuwa ikitoa mafunzo kwa watendaji wa klabu ili waweze kufanya kazi zao vizuri na kwa mintaarafu ya mpira wa miguu na hivyo kuondolewa kwa timu nzima kama hiyo kunamaanisha kuwa ni upotevu wa rasilimali ambayo imetumika kuwapa elimu ya kutenda kazi zao vizuri.

TFF ilishafanya kozi ya Event Management kwa ajili ya watendaji wa klabu; semina ya kuangalia upya maazimio ya Bagamoyo kwa watendaji na viongozi na pia kozi ya utawala hivyo haipendi juhudi hizi zipotee kirahisi.

No comments:

Post a Comment