Thursday, September 27, 2012

FALCAO NOMA... ATUPIA MBILI KUIPAISHA ATLETICO MADRID HADI NAFASI YA PILI KATIKA MSIMAMO WA LA LIGA... SASA AWABURUZA KWA MABAO MESSI, CRISTIANO RONALDO

Goooooohh..! Straika Falcao akishangilia goli alilotupia
Radamel Falcao

MADRID, Hispania
Radamel Falcao alifunga mara mbili wakati Atletico Madrid ikicharuka kutoka kuwa nyuma na kushinda ugenini kwa mabao 4-2 dhidi ya Real Betis, hivyo kupanda hadi nafasi ya pili katika msimamo wa La Liga, Ligi Kuu ya Hispania jana usiku.

Straika huyo wa kimataifa wa Colombia aliye katika kiwango cha juu aliongeza idadi ya mabao yake na kufikia saba katika mechi tano baada ya kupiga shuti lililokwenda wavuni na kuongeza jingine la penati mara baada ya mpira kuanzishwa tena, hivyo kujiweka kileleni mwa wafungaji wanaoongoza kwa mabao katika La Liga huku akiwaacha nyota Lionel Messi wa Barcelona mwenye mabao sita na Cristiano Ronaldo aliyefikisha mabao matatu.

Watokea benchi Diego Costa na Raul Garcia walikamilisha ushindi wa Atletico Madrid wakati Betis walipomaliza mechi wakiwa tisa uwanjani na kuwasaidia mabingwa wa Ligi ya Europa (Atletico Madrid) kufikisha pointi 13 kutokana na mechi tano, pointi mbili kabla ya kuwashika vinara Barcelona.

Betis walipata goli la utangulizi katika dakika ya 25 wakati mpira wa krosi ya Salvador Agra ulipodunda ndani ya eneo la hatari na beki wa Atletico, Miranda akajifunga katika harakati za kuokoa.

Iliwachukua dakika mbili tu Atletico kusawazisha bao hilo baada ya Falcao kuiwahi krosi ya chini ya Raul Garcia na kufunga.

Kipa wa Betis, Casto Espinosa aliiokoa timu yake mara kadhaa na kabla ya mapumziko wakaongoza tena, safari hii krosi ya Juan Carlos ikaenda moja kwa moja wavuni baada ya kumpita beki Juanfran wa Atletico.

Atletico wakasawazisha tena kwa haraka. Falcao akaangushwa na refa akatoa penati mara tu baada ya mpira kuanzishwa, uamuzi uliopingwa na wachezaji wa Betis ambao mwishowe ulimfanya beki wao Damien Perquis apewe kadi nyekundu ya kiaktili, na Mcolombia Falcao akafunga penati hiyo.

Falcao, aliyekuwa akisumbuliwa na maumivu ya paja kabla ya mechi hiyo, alitolewa na nafasi yake ikatwaliwa na Costa na mshambuliaji huyo Mbrazil akaipa tena uongozi Atletico kutokana na mpira wa kona.

Wenyeji wakajikuta kwenye wakati mgumu zaidi wakati mtokea benchi Joel Campbell alipotolewa nje kwa kadi ya pili ya njano katika dakika ya 83.

Raul Garcia aliifungia Atletico bao la nne na kuiacha Betis ikiwa katika nafasi ya sita kutokana na pointi tisa baada ya kumalizika kwa mechi hiyo iliyoahirishwa awali mwanzoni mwa mwezi huu.

No comments:

Post a Comment