Tuesday, August 14, 2012

WENGER ASEMA PIGA UA.... PODOLSKI LAZIMA AMPANGE KATIKA KIKOSI KITAKACHOFUNGUA DIMBA LIGI KUU YA ENGLAND DHIDI YA SUNDERLAND

Lukas Podolski akionekana mwenye furaha tele ndani ya 'uzi' wa klabu yake mpya ya Arsenal.... hilo tambara mkononi la kupinga ubaguzi wa rangi linamfanya aonekane kama nd'o mrithi wa nahodha Van Persie vile!

Lukas Podolski .... waleteni hao Sunderland!

Podolski (kulia) akimtoka beki mmojawapo wa Koln katika mechi yao ya kirafiki Jumapili iliyopita nchini Ujerumani ambayo Podolski alifunga mara mbili na kuisaidia Arsenal kushinda 4-0.

Straika Podolski akishangilia baada ya kutupia bao lake la kwanza dhidi ya Koln
KOLN, Ujerumani
KOCHA wa Arsenal, Arsene Wenger amefichua leo kwamba straika wake mpya, Lukas Podolski ana "nafasi kubwa sana" ya kuwemo katika kikosi chake kitakachoshuka dimbani kucheza mechi ya ufunguzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu ya England dhidi ya Sunderland.

Nyota huyo wa kimataifa wa Ujerumani alifunga mabao mawili Jumapili dhidi ya Koln, timu aliyoihama na kutua Arsenal katika kipindi hiki cha uhamisho wa majira ya kiangazi, na kocha wake mpya amekunwa na kiwango kilichoonyeshwa na straika huyo katika mechgi zao za maandalizi ya msimu.

Hata hivyo, Wenger alikiri kwamba Podolski bado hajawa 'fiti' kwa asilimia zote baada ya kuongezewa siku za kupumzika baada ya kumalizika kwa fainali za Euro 2012, lakini bila kujali hilo, amesema anaamini kuwa mchezaji huyo mwenye miaka 27 atakuwa tayari kucheza na kuisaidia timu yake katika mechi yao ya ufunguzi wa ligi kuu.

"Tunaridhishwa sana na kiwango chake," Wenger aliwaambia waandishi wa habari nchini Ujerumani baada ya kumalizika kwa mechi yao dhidi ya Koln.

"Kwa vyovyote vile atakuwemo kikosini (dhidi ya Sunderland) na ana nafasi kubwa ya kuanza katika kikosi kitakachocheza mechi hiyo.

"Kimwili hayuko fiti kwa asilimia 100. Kiasi bado hajawa na kasi lakini hilo tutalishughulikia. Tunajua kwamba anaweza kufunga mabao."

Uwezekano wa nahodha Robin van Persie kucheza katika mechi hiyo uko shakani kufuatiua kuendelea kwa uvumi mwingi kuhusiana na hatma yake klabuni hapo.

Hiyo inamaanisha kwamba jukumu kubwa la ushambuliaji sasa limebaki kwa Podolski, lakini nyota huyo wa zamani wa Bayern Munich alicheza upande wa kushoto wa mpinzani wake mpya kikosini, Olivier Giroud wakati wakicheza dhidi ya Koln kwenye Uwanja wa RheinEnergie.

No comments:

Post a Comment