Wednesday, August 1, 2012

KAFULILA AIRARUA BAJETI YA DK. MWAKYEMBE


*AHOJI KWANINI TAIFA LINAKOSA NDEGE HUKU RWANDA IKIWA NAZO SABA? KWANINI BADO TUNATUMIA RELI ILIYOCHOKA NA MELI CHAKAVU KAMA MWONGOZO ILIYONUNULIWA KARNE YA 18?

Mhe. David Kafulila

Mhe. Dk. Harrison Mwakyembe

Hamad... dege la Shirika la Ndege Tanzania (ATC) likionekana sakafuni baada ya kupata ajali mkoani Kigoma. 

Polisi wakiilinda ndege ya ATC iliyopata ajali mkoani Kigoma April, 2012. Kwa ndege kama hii, kwanini Kafulila asihoji suala la kuboresha usafiri wa anga?

Baadhi ya wananchi mkoani Kigoma wakiteremka kutoka kwenye meli ya Mv Mwongozo iliyonunuliwa na wakoloni kabla ya uhuru mwaka 1961... Kafulila anaitilia shaka meli hii kwa kudai kwamba sasa imechakaa mno!



Mbunge wa Kasulu Kusini,  David Kafulila (NCCR-Mageuzi), ameijia juu serikali na kutaka iwekeze vya kutosha katika kuimarisha miundombinu ya reli, ndege na meli ili hatimaye maisha ya Watanzania yaboreshwe na pia kuonyesha sababu za msingi za kuwaondoa wakoloni.

Kafulila ameyasema hayo bungeni  jioni hii wakati akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi inayoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe.

Alisema kuwa inasikitisha kuona kuwa hata baada ya miaka zaidi ya hamsini ya uhuru, Tanzania bado inategemea mioundombinu ya karne ya 18 iliyoachwa na wakoloni na kurudisha nyuma kasi ya wananchi katika kujiletea maendeleo.

Akitoa mfano, Kafulila alisema kuwa Tanzania ambayo ni nchi kubwa na yenye utajiri mkubwa wa rasilimali na pia ikijivunia hali ya amani na utulivu tangu ilipopata uhuru, bado inapitwa na nchi ndogo kama Rwanda katika usafiri wa ndege, licha ya kwamba nchi hiyo ni ndogo na tena inayokabiliwa na misukosuko mingi ya kisiasa na vita vya wenyewe kwa wenyewe.

 "Leo hii Rwanda ina ndege saba zinazofanya safari hadi hapa kwetu, sisi Tanzania hatuna ndege... kwanini?"

Kafulila alieleza kuwa inasikitisha kuona kwamba hadi sasa, wananchi wa Kigoma wanaendelea kutegemea usafiri wa meli ya Mv.Mwongozo kwenye Ziwa Tanganyika, ambayo ilinunuliwa na wakoloni kabla ya uhuru na sasa imechakaa mno, akitoa mfano kwa kusema kuwa: " mtu akipanda leo saa 8:00, anafika kesho... ni kwa sababu imezeeka."

Alisema kuwa Baba wa Taifa, Mwl. Nyerere alipigania uhuru kwa sababu wakoloni walikuwa wanachelewesha maendeleo, lakini mpaka sasa taifa linaendelea kutumia miundombinu ileile iliyojengwa na kununuliwa na wakoloni toka karne ya 18 wakati hivi sasa ni karne ya 21.



"Sasa kama bado tumebaki na vitu vilevile katika karne hii ya 21, kwanini basi tuliwaondoa wakoloni?" Alihoji na kushangiliwa na wabunge wengi, hasa wenzake wa upinzani.


Kati ya mambo ambayo Dk. Mwakyembe ameahidi kuyatekeleza katika bajeti ya wizara yake kwa mwaka ujao wa fedha ni pamoja na kununua ndege mbili za Shirika la Ndege Tanzania. 

No comments:

Post a Comment