Tuesday, July 24, 2012

WAZIRI ALIYEJIUZULU KWA KUZAMA BOTI YA MV SKAGIT APONGEZWA


Mhe. Hamad Masoud Hamad

Chama cha Wananchi (CUF) kimeungana na wananchi wengine mbalimbali kumpongeza Mhe. Hamad Masoud Hamad kwa hatua yake ya kujiuzulu nafasi ya kuwa Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwa ni siku chache tu baada ya kuzama kwa boti ya Mv Skagit na kuua mamia ya watu.


Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Sera wa CUF, Salum Dimani, amesema kuwa chama chao, ambacho ndicho anachotoka Mhe. Hamad, kimebaini kuwa waziri huyo wa zamani hakufanya kosa lolote, bali amechukua hatua hiyo kwa nia ya kuwajibika kisiasa; hatua ambayo wametaka iigwe na viongozi wengine wa juu pindi matukio ya namna hiyo yanapotokea.  


Hamad alitangaza rasmi hatua yake ya kujiuzulu jana na kusema kuwa aliandika barua hiyo tangu Julai 20 (siku moja baada ya boti kuzama), lakini alitakiwa na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein kuwa afanye subira na jana ndipo akakubaliwa.


Jana, Dk. Shein alimteua Mwakilishi wa Jimbo la Ziwani (CUF), Rashid Seif Suleiman kuwa mrithi wa nafasi ya Hamad katika kuongoza wizara hiyo ya Miundombinu na Mawasiliano.

No comments:

Post a Comment