Tuesday, July 24, 2012

KADA CCM AKUTWA LEO NA HATIA WIZI WA FEDHA ZA EPA, AFUNGWA MIAKA MITATU

Maranda (kulia) na Farjala.

Farjala (kushoto) na Maranda (mbele kushoto) wakisindikizwa katika korido za Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam imewahukumu kwenda jela miaka 18 wafanyabiashara na ndugu wawili, Rajabu Maranda ambaye alikuwa mweka hazina wa CCM mkoani Kigoma na Farijala Hussein, baada ya wote kupatikana na hatia ya makosa sita kati ya saba waliyokuwa wanakabiliwa nayo, yakiwemo ya kujipatia Sh bilioni 2.2 za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Licha ya kutakiwa kwenda jela miaka 18, watatumikia miaka mitatu jela ambayo itakwenda sambamba pamoja na kifungo cha awali cha miaka mitano kutokana na kifungo cha miaka mitatu kwa kila kosa, ambayo ni kula njama, kughushi nyaraka, kuwasilisha hati bandia na kujipatia Sh. 2,266,049,041.25.

Mahakimu  waliosikiliza kesi hiyo walikuwa na hukumu mbili tofauti. Ya kwanza iliandaliwa na Mwenyekiti wa jopo la mahakimu hao, Fatuma Masengi ambaye ni Jaji wa Mahakama Kuu aliyepewa kibali na Jaji Mkuu Tanzania kusikiliza kesi hiyo ambaye aliona washtakiwa hao hawana hatia.


Hukumu nyingine iliyotumika na mahakama imeandaliwa na mahakimu wawili, Projestus Kahyoza na Katalina Revocat -- hii iliwatia wote wawili hatiani kwenye makosa sita kati ya saba yaliyokuwa yakiwakabili.



Hakimu Kahyoza alisema wakati akisoma hukumu hiyo kuwa, baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi saba wa upande wa mashtaka, mahakama imeona kuwa pasi na shaka, washtakiwa hao wana hatia katika makosa sita kati ya saba.


Alisema upande wa mashtaka umeweza kuthitisha shtaka la kula njama kwa kuwa katika maelezo ya onyo ya mshtakiwa Hussein ambayo yalipokelewa kama kielelezo na mahakama hiyo, yanaeleza kuwa alipewa maelekezo na ndugu yake Maranda kuhusu kuandaa nyaraka za kughushi jina la kampuni pamoja na mahali ambapo ofisi ya kampuni hiyo itakuwepo.

  
 “Katika ushahidi ulitolewa na Jamhuri hapa mahakamani, hakuna ubishi kama washtakiwa walighushi nyaraka za kusajili jina la kampuni kutumia majina ya Paul Tobias na Fundi Kitunga, mahakama hii inaamini shtaka hili kweli washtakiwa walighushi nyaraka hizo.”


Akielezea shitaka la kuwasilisha nyaraka bandia, Hakimu Kahyoza alisema washtakiwa waliwasilisha nyaraka hizo wakati huo (United Bank of Afrika (UBA) ambapo walifungua akaunti ya pamoja. Alisema kwa kutumia majina ya uongo (Paul na Fundi), mahakama inaamini washtakiwa walighushi hati ya kuhamisha deni wakionyesha ni wakala kutoka Kampuni ya   B.Graciel ya Ujerumani kwenda Kampuni ya Money Planers & Consultant ya Tanzania.


Hakimu huyo alisema kuwa mahakama inaamini washtakiwa waliwasilisha BoT hati za kughushi kwa ajili ya maombi ya Sh. bilioni 2.2 ambazo walifanikiwa kuhamishiwa kupitia akaunti yao iliyokuwa benki ya UBA. Aliongeza kuwa: "Mahakama inawaona washtakiwa hao hawana hatia kwenye shtaka la sita la wizi ambalo hakuna shahidi wa upande wa Jamhuri aliyethibitisha kama washtakiwa waliibia BoT.”

Aliongeza kwamba kutokana na maelezo yote hayo hakuna ubishi kwamba washtakiwa walijipatia fedha kwa njia ya udanganyifu baada ya kula njama, kughushi nyaraka na kuwasilisha hati bandia BoT. Kwa upande wa Hakimu Masengi alisema katika hukumu yake ambayo itakuwa kumbukumbu ya mahakama, ameona ushahidi uliotolewa na washtakiwa hauna nguvu ya kuwatia hatiani na kwamba jukumu la kuthibitisha kesi ni la Jamhuri.

 
Alisema katika kesi hiyo, BoT haijafika mahakamani hapo kueleza au kulalamika kama waliibiwa fedha hizo na hata ile kampuni ya B.Graciel ya Ujerumani hawajalalamika kuibiwa fedha hizo na washtakiwa. Hakimu Masengi alisema Wakala wa Majina ya Biashara (Brela) hawajalalamika kupokea nyaraka zilizoghushiwa na washtakiwa mahakamani hapo na kwamba ushahidi huo wa Jamhuri unaonyesha ni jinsi gani wameshindwa kuondoa mashaka mbele ya mahakama hiyo.

Hakimu Revovat alisoma hukumu hiyo kwamba washtakiwa wataanza kutumikia kiifungo hicho kuanzia jana sambamba na kifungo cha awali. Katika kesi hiyo,washtakiwa wanadaiwa kuwa Machi 20 na Desemba 25, mwaka 2005 washitakiwa walijipatia ingizo la Sh. 2,266,049,041.25 wakidai kwamba Kampuni ya B.Graciel ya Ujerumani imehamishiwa deni na Kampuni ya Money Planers & Consultant ya Tanzania.

No comments:

Post a Comment