Tuesday, July 31, 2012

WALIMU WALIOGOMA JIJINI DAR WATAKIWA KUJIELEZA


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiq
Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam, Said Mecky Sadiq, amewaagiza wakurugenzi wa manispaa za Ilala, Temeke na Kinondoni kuwaandikia barua za kuwataka kujieleza walimu wote waliokosekana kwenye vituo vyao vya kazi jana katika siku ya kuanza kwa mgomo usio na kikomo uliotangazwa na Chama cha Walimu Tanzania (CWT).

Akizungumza na waandishi leo, mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa mgomo huo si halali na kwamba, walimu wote waliouunga mkono watachukuliwa hatua.

Akitoa tathmini ya mahudhurio ya walimu jana, Sadiq alisema kuwa hali haikuwa mbaya sana katika shule za msingi kulinganisha na sekondari.

Alisema kwamba katika Manispaa ya Temeke, walimu walioshiriki mgomo jana ni 1,484 ambao ni sawa na asilimi 34, Kinondoni waligoma walimu 2,074 na waliogoma Ilala ni walimu
107 tu, ambao ni sawa na asilimia 5.95.


NAIBU WAZIRI PHILLIP MULUGO
Naibu Waziri wa Elimu na na Mafunzo ya Ufundi, Phillip Mulugo, alifanya ziara ya ghafla mkoani Morogoro na kuangalia athari za mgomo katika baadhi ya shule, zikiwamo za sekondari Morogoro, sekondari Kilakala na Shule ya Msingi Mwere.

Naibu Waziri huyo alikuta walimu 45 wa sekondari Morogoro wamegoma na alipofika katika shule ya Mwere, alikuta wanafunzi wengi wakiwa nje ya madarasa baada ya walimu kukosekana madarasani.

Hata hivyo, Mulugo alikuta walimu wa shule ya Kilakala wakiendelea na kazi kama kawaida huku katibu wa Tawi la CWT shuleni hapo akisema kuwa wao hawaungi mkono mgomo huo.

Jana, walimu nchini walianza mgomo usio na kikomo uliotangazwa na CWT kwa nia ya kuishinikiza serikali kuwatekelezea madai yao kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwaongezea mishahara kwa asilimia 100.

No comments:

Post a Comment