Thursday, July 26, 2012

TUTAMLETA MSAIDIZI WA SUNZU - KABURU

Geofrey Nyange 'Kaburu'

Na Somoe Ng'itu
UONGOZI wa klabu ya Simba umewataka mashabiki wa timu yake kutokata tamaa baada ya kuondolewa katika mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati na sasa wanajipanga kuhakikisha kuwa wanafanya vizuri katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara utakaoanza Septemba Mosi.


Mabingwa hao wa Bara waliiaga michuano ya Kombe la Kagame Jumanne baada ya kufungwa magoli 3-1 na Azam katika mchezo wa robo fainali uliochezwa Jumanne kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.


Akizungumza na STRAIKA leo, Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange 'Kaburu', alisema kuwa Kamati ya Ufundi ya klabu hiyo inakutana kufanya tathmini ya timu yao na kikubwa ni kujaza nafasi ambazo zimeonekana zina mapungufu kabla ya kuanza kwa msimu ujao wa ligi.


Kaburu alisema kuwa kikosi cha Simba kina wachezaji wapya ambao walikuwa wakihitaji muda wa kujiandaa zaidi, jambo ambalo ndio lililowasumbua wakiwa kwenye michuano hiyo.


"Tunajipanga na tutahakikisha makosa yaliyoonekana katika mashindano ya Kagame yanafanyiwa kazi. Tusikate tamaa, Simba itakuwa bora msimu ujao licha ya kikosi kuondokewa na wachezaji muhimu," alisema kiongozi huyo.


Alisema katika usajili wao, watahakikisha wanaongeza beki mwingine wa kati aliye na uwezo pamoja na mshambuliaji ambaye atasadiana na Felix Sunzu katika ufungaji.


Wakati huo huo, tawi la Simba la Mpira Pesa lililoko Magomeni jijini Dar es Salaam, Jumapili litakuwa na mkutano wa wanachama wake ambapo wamepanga kujadili ushiriki wa timu yao kwenye mashindano ya Kombe la Kagame.

No comments:

Post a Comment