Thursday, July 26, 2012

USALAMA WA TAIFA WAKANA KUMTEKA DK. ULIMBOKA


Mhe. George Mkuchika, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora)
Idara ya Usalama wa Taifa imekanusha taarifa zinazowahusisha na tukio la kutekwa, kuteswa na kumtupa kwenye msitu wa Mabwepande jijini Dar es Salaam kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Steven Ulimboka.

Taarifa iliyotolewa leo na idara hiyo imeeleza kuwa habari zinazodai kwamba ndio waliohusika kumteka Dk. Ulimboka ambaye hivi sasa anaendelea na matibabu nchini Afrika Kusini na nyingine zinazodai kuwa wana mpango wa kuwadhuru watu mbalimbali si za kweli, na kwamba wanaozisambaza wana lengo la kuichafua taasisi hiyo nyeti kwa usalama wa taifa.

Kwa sababu hiyo, taarifa hiyo imewataka wananchi kupuuza taarifa hizo, na kuwahakikishia Watanzania kuwa 'uzushi' huo hautawavunja moyo.

Imeeleza zaidi kwamba badala yake, Idara ya Usalama wa Taifa itaendelea kushirikiana na wananchi na vyombo vingine vya usalama katika kuhakikisha kuwa wakati wote nchi inakuwa salama.

Taarifa hiyo imetolewa leo ikiwa ni siku moja tu baada ya gazeti la Mwanahalisi la jana Jumatano (Julai 25, 2012) kuwatuhumu watu wa usalama wa taifa kuhusika na tukio la kumteka Dk. Ulimboka.
Katika habari hiyo, Mwanahalisi liliwataja kwa majina baadhi ya watu waliodaiwa kuwa ni maafisa wa idara hiyo waliohusika kumteka Dk. Ulimboka.

Dk. Ulimboka aliyekuwa mstari wa mbele katika harakati za mgomo wa madaktari uliotokea hivi karibuni, alidaiwa kutekwa na watu wasiojulikana na kuumizwa vibaya kabla ya kukutwa kwenye msitu wa Mbawepande.

Kamanda wa Polisi katika Kanda Maalum ya Dar es Slaam, Suleiman Kova alimtaja Mkenya Joshua Mhindi kuwa ndiye mtuhumiwa aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo, akieleza kwamba walimtia mbaroni baada ya kubaini kuwa alikwenda katika Kanisa la Wokovu na Uzima la Mchungaji Gwejima lililopo Kawe jijini Dar es Salaam kwa nia ya kuungama huku akikiri kufanya tukio hilo na wenzake wa kundi la Gun Star.

Idara ya Usalama wa Taifa iko chini ya Wizara ya Nchi katika Ofisi ya Rais (Utawala Bora), ambayo inaongozwa na Mhe. George Mkuchika.

No comments:

Post a Comment