Friday, July 20, 2012

TAZAMA JAMAA ALIVYOPIGWA BUTWAA BAADA YA KUKOSA NDUGU ZAKE WAWILI WALIOPANDA BOTI YA SKAGIT LAKINI HAWAMO KATIKA ORODHA YA WATU 340 ILIYOKABIDHIWA SERIKALINI NA WAMILIKI WA CHOMBO HICHO

George akiwa mwenye huzuni tele katika ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam leo baada ya kukagua majina ya watu waliozama na boti ya Mv Skagit na kutoona majina ya jamaa zake wawili kutoka Kenya ambao aliwasindikiza kupanda chombo hicho.

Hapa George anaelezea machungu yake kwa waandishi wa habari katika ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam leo baada ya kufika ili kukagua majina ya jamaa zake wawili waliozama na meli ya Mv Skagit na kutoyaona wakati akiwa na uhakika kuwa walikuwamo ndani ya chombo hicho.

George akiendelea kuwafafanulia waandishi wa habari katika ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam leo juu mshangao wake wa kutoona majina mawili ya jamaa zake wawili kutoka Kenya waliopanda boti iliyozama juzi ya Skagit. 

Severine George, mkazi wa jijini Dar es Salaam yuko njiapanda. Ni baada ya jamaa zake wawili ambao ni raia wa Kenya kutokuwamo katika orodha ya majina 340 iliyotolewa na Serikali leo na kuelezwa kuwa ndio waliokuwamo ndani ya boti ya Skagit wakati ikizama juzi kwenye eneo la Chumbe wakati ikitokea jijini Dar es Salaam kuelekea visiwani Zanzibar.

Akizungumza na Straika katika ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam leo ambako ndiko orodha ya watu hao ilikobandikwa na wananchi wenye ndugu zao kupewa fursa ya kwenda kuiona, George anasema kuwa ameshangazwa kwa kutowaona jamaa zake aliowataja kwa majina ya Mary Kiyoko na Benard Kalii.

Kwa sababu hiyo, George anasema kuwa amechanganyikiwa na hajui awaambie nini ndugu walioko Kenya, ambao kila mara wamekuwa wakimpigia simu kutaka kujua hatma ya watu hao.

Akieleza zaidi, George anasema kuwa juzi, yeye alishiriki kuwasindikiza jamaa zake hao waliokuwa watatu na wote waliingia ndani ya boti ya Skagit kuelekea Zanzibar.

Hata hivyo, anasema kuwa baada ya tukio la kuzama kwa boti hiyo, aliyetambuliwa hadi sasa akiwa marehemu ni mwanamke mmoja ambaye alimtambua kirahisi kwa vile anakumbuka namna alivyosuka nywele zake kwa kuzifunga rasta.

“Baada ya kutoonekana kwa hawa wawili (Kiyoko na Kalii), leo nd’o nikadamkia hapa (katika ofisi za Mkuu wa Mkoa) ili niione orodha na kujua hatua za kuchukua kulingana na maelekezo yaliyotolewa na serikali,” anasema George.

“Hata hivyo, nimeshangazwa kuona kuwa katika orodha yote hii ya majina yaliyoletwa na wenye boti (ya Skagit), sijaona jina la Mary wala Benard… hapa nimechanganyikiwa.  Simu kutoka Kenya kuulizia hatma yao zimekuwa nyingi na sijui  cha kuwajibu,” anasema George.

Akielezea kile anachodhani kuwa ndio chanzo cha kutokea tatizo hilo la kutoonekana kwa baadhi ya majina, George anasema kuwa ni mfumo mbovu uliokuwapo wa ukatishaji tiketi na uingiaji wa abiria ndani ya boti hiyo kabla haijatoa nanga yake kwenye bandari ya Dar es Salaam.

Anaema kuwa kuwa hadi sasa, pale bandarini (Dar es Salaam) sijaona ofisi rasmi za boti ya Skagit na kwamba, kilichotokea, wenye kutaka kusafiri walikuwa wanapewa tiketi na watu waliokuwa katika eneo la bandari wakiwa na makabrasha ya tiketi za boti hiyo.

“Kwa utoaji tiketi wa aina hii, wakati mwingine unaweza kuitwa Severine lakini tiketi unayopewa ikawa imeandikwa Hassan…  hapo kuingia kwenye boti huwa hakuna shida kwa sababu kinachoangaliwa ni tiketi tu,” anasema George.

“Binafsi, kwa idadi ya watu niliowaona siku ile sidhani kama walikuwa wa idadi hii inayotajwa (340), nadhani walizidi sana,” anasema.

George akavishauri vyombo vya dola kufuatilia suala hilo kwa undani zaidi kwani kwa kutowaona jamaa zake wawili waliopanda boti hiyo, anadhani kwamba huenda kuna watu wengine wengi waliokuwamo kwenye chombo hicho lakini wakakosekana kwenye orodha hiyo ya watu 340.    

Hadi kufikia jana saa 1:00 usiku wakati zoezi la uokoaji likisitishwa, watu waliookolewa wakiwa hai walifikia 146 na miili iliyoopolewa kufikia 52, ikiwemo miili 37 iliyoopolewa jana.

Serikali zote mbili, ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi Zanzibar zilitangaza siku tatu za maombolezo kuanzia jana.

No comments:

Post a Comment