Thursday, July 12, 2012

HALIMA MDEE APIGWA BITI KALI NA SPIKA


Mhe. Halima Mdee (aliyeinua mkono) akiwa bungeni.
Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai amempa onyo kali Mbunge wa Kawe kwa tiketi ya Chadema, Mhe. Halima Mdee kutokana na kile alichodai kuwa ni tabia yake ya kutoheshimu kiti cha spika.

Mhe. Ndugai alichukua hatua hiyo baada ya kukerwa na kitendo cha Mhe. Halima kutaka kutoa taarifa wakati yeye akiendelea kutoa mwongozo wake dhidi ya tuhuma za Mbunge wa Kigamboni, Mhe. Dk. Faustine Ndungulile, aliyekuwa akisomewa hukumu yake kutokana na kosa la kutoa tuhuma zisizokuwa na ushahidi dhidi ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka.

Ndugai alisema kuwa Mhe. Halima amekuwa na tabia ya kutoheshimu kiti cha Spika kwa kuzungumza bila kupata idhini na kwamba, anachukua fursa hiyo kumpa onyo la mwisho kwani ni kinyume cha taratibu za mabunge yote.

Wakati Mhe. Ndugai akiendelea kutoa maelezo yake, Mhe. Halima alionekana akifanya jitihada za kupata nafasi ya kutoa hoja yake kwa kutamka neno “taarifa”. Jambo hilo likamkera zaidi Mhe. Ndugai ambaye sasa alionekana kuongea kwa ukali na kumuamuru akae chini.

Baada ya hapo, Mhe. Ndugai akazidi kumshutumu Mhe. Halima na kusema kwamba wananchi wa Kawe wanajionea mbunge wao, akisema ni “kituko tu”.
Akamwambia zaidi kwamba anajua kuwa (Mhe. Halima) anataka umaarufu tu kwa kutolewa nje ya ukumbi (kama ilivyokuwa kwa Ndungulile) ili kesho yake magazeti yote yamuandike. 

Kwa kutambua hilo, Ndugai akadai kuwa yeye (Mhe. Halima) hamtoi nje  na badala yake anampuuza tu.

Hayo yote yametokea jioni hii Bungeni Dodoma wakati wa kuhitimisha mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.


No comments:

Post a Comment