Thursday, July 12, 2012

MBUNGE KIGAMBONI ATIMULIWA BUNGENI, ASIMAMISHWA VIKAO VITATU


Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai
Mbunge wa Kigamboni kwa tiketi ya CCM, Mhe. Dk. Faustine Ndungulile amejikuta akitimuliwa bungeni mjini Dodoma jioni hii na kutolewa na askari hadi nje ya ukumbi baada ya kushindwa kuwasilisha ushahidi wa madai aliyotoa awali kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi (Prof. Anna Tibaijuka) alitumia fedha za serikali kuwapeleka bungeni hapo baadhi ya wananchi wa Kigamboni ikiwa ni sehemu ya jitihada za kusaka uungwaji mkono wa mradi wa mji wa Kigamboni.

Aliyetoa amri ya kutimuliwa kwa Mhe. Ndungulile ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai; ambaye alisema kwamba kitendo alichofanya mbunge huyo hakikubaliki kwani ni kinyume cha kanuni za Bunge.

Mhe. Ndungulile alitoa tuhuma hizo jana wakati akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Baada ya hapo, Mhe. Ndugulile akaamriwa kuwasilisha ushahidi wa madai yake leo jioni na aliposhindwa kufanya hivyo, ndipo Mhe. Ndugai alipomtimua nje ya ukumbi na pia kumsimamisha kwa kumuamuru kuwa asihudhurie katika vikao vitatu vijavyo vya Bunge kutokana na kosa hilo la kusema uongo bungeni

Mara baada ya Mhe. Ndugai kutoa hukumu hiyo, Ndungulile alionekana kutii amri kwa kutoka nje ya ukumbi huku akisindikizwa na askari walioamrishwa kufanya hivyo na kiti cha spika.

No comments:

Post a Comment