Salama Jabir (kulia) pamoja na majaji wenzake wa EBSS, Ritha Paulsen (katikati) na Master Jay wakiendesha mchakato wa kusaka vipaji vya kuimba mjini Mbeya. |
Na Mwandishi Wetu, Mbeya
MAJAJI wa shindano la Epiq Bongo Star Search (EBSS) pamoja na washiriki wao mkoani Mbeya jana walisimama kwa dakika mbili kukumbuka watu waliopoteza maisha katika ajali ya bori ya Mv Skagit iliyotokea hivi karibuni ambapo watu wengi walipoteza maisha.
Ilikuwa katika ukumbi wa Vibe uliopo Mbeya ambapo mara tu baada ya kuwasili ukumbini hapo majaji hao wakiongozwa na Jaji Mkuu, Ritha Paulsen walionesha kusikitishwa kwao na ajali hiyo.
Akizungumzia ajali hiyo muda mfupi kabla ya kuanza kusikiliza vipaji vya washiriki wa mkoani Mbeya, Ritha alisema kuwa akiwa kama mdau wa muziki anaungana na Watanzania wote kwa ujumla kuomboleza msiba huo mkubwa.
Alisema anaamini kuwa katika watoto waliopoteza maisha katika ajali hiyo wapo ambao walikuwa na ndoto ya kuwa wanamuziki wa baadae na hivyo akiwa kama mdau wa sanaa ya muziki anaona kuwa ni sawa na amepoteza vipaji vingi.
"Si tu kama tumeguswa na msiba huu bali umetuathiri kama wadau wa muziki, na taifa zima kwa ujumla, na tunawaombea walazwe pema wale wote waliopoteza maisha na ajali hii," alisema Ritha.
Naye Afsa Biashara Mkuu wa Zantel, Sajid Khan, aliungana na majaji katika kuomboleza msiba huo, akisema, wao kama Zantel wameguswa sana na msiba huo, na wanaungana na Watanzania wote katika kuomboleza msiba huo.
"Msiba huu ni wetu sote Watanzania, na ndio maana sisi kama Zantel tumetenga muda wa kuwaombea watu waliopoteza maisha yao katika ajali hii," alisisitiza Khan.
Katika usaili wa mkoani Mbeya uliohudhuriwa na mamia ya washiriki, vipaji vingi vilianza kuonekana mapema kutokana na washiriki wake wengi kuonekana kuanza vema katika uimbaji.
Akizungumzia mkoa wa Mbeya katika suala la uimbaji wa muziki, Ritha alisema kuwa kutokana na sifa iliyonao mkoa huu ya kupenda na kuumudu muziki wa Injili anaona kuwa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kupata pia vipaji vya muziki wa kidunia.
“Najua kuwa wasanii wengi wa muziki wa Injili wanaotamba wanatoka mkoani hapa sasa ni imani yangu kuwa kupitia EBSS tunaweza kuvipata vipaji vya muziki vya kawaida na kuviendeleza zaidi kimataifa,” alisema Ritha.
No comments:
Post a Comment