Sunday, March 10, 2013

SIMBA ILIYOWATOSA MASTAA WAKE KIBAO YAFUFUA MATUMAINI KWA KUIPIGA COASTAL UNION 2-1… KASEJA, JUMA NYOSSO, KOMABIL KEITA, KAZIMOTO, MZAMBIA FELIX SUNZU NA HARUNA MOSHI ‘BOBAN’ NI MIONGONI MWA NYOTA WALIOACHWA NJE YA KIKOSI CHA LEO

Mrisho Ngassa (kulia) akijaribu kuwatoka wachezaji wa Coastal wakati wa mechi yao ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo.


Wachezaji kibao wa kikosi cha pili cha Simba walionyesha kiwango cha juu na kufufua matumaini yao ya kuikamata Azam baada ya kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Coastal Union ya Tanga katika mechi yao kali ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo.

Kipa chaguo la kwanza Juma Kaseja aliyeonekana jukwaani akiwa na mashabiki wengine wa kawaida, mabeki Juma Nyosso na Komalbil Keita, viungo Mwinyi Kazimoto na Haruna Moshi 'Boban'; na straika wa kimataifa kutoka Zambia, Felix Sunzu ni miongoni mwa nyota wa kikosi cha kwanza cha Simba walioachwa nje katika siku ambayo taarifa zilishazagaa mitaani kuwa majina ya wakali kibao yalikabidhiwa na uongozi kwa kocha Mfaransa Patrick Liewig wakidaiwa kuwa wanaihujumu timu na hivyo aamue mwenyewe kuwapanga ama la.

Wakiongozwa na Mrisho Ngassa, Nassoro Masoud 'Chollo' na Shomari Kapombe, kikosi kilichojaa yosso cha Simba kiliwashangaza wengi kwa magoli mawili ya haraka katika dakika tatu za majeruhi kabla ya mapumziko.

Ngassa aliifungia Simba goli la kuongoza katika dakika ya 45 baada ya kuuwahi mpira uliotemwa na kipa Shaaban Kado kufuatia shuti kali la Abdallah Seseme na Haruna Chanongo akaongeza la pili muda mfupi kabla refa Martin Saanya hajapuliza filimbi ya mapumziko.

Coastal walikianza kwa kasi kipindi cha pili na walihitaji dakika nne tu kupata goli lao kupitia Razak Khalfan aliyetumia vyema pasi ya Mohamed Athuman.

Tukio la huzuni kwa Simba ni kuumia kwa Jonas Mkude aliyelazimika kutolewa uwanjani kwa machela katika dakika ya 80 na nafasi yake kuchukuliwa na Mussa Mude.

Ushindi huo ulimaanisha kwamba Simba waliocheza mechi 19 wamejihakikishia kubaki katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi wakiwa na pointi 34, tatu juu ya Coastal, Mtibwa na Kagera Sugar zilizocheza mechi 20 kila moja.

Yanga inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 45, nane zaidi ya Azam iliyoshikiliwa kwa sare na Polisi Morogoro jana huku kila moja ikishuka dimbani mara 19.

Vikosi:
Simba:- Abel Dhaira, Nassoro Masoud 'Chollo', Miraji Adam, Hassan Khatib, Shomari Kapombe, Jonas Mkude/Mussa Mude (dk. 80), Amri Kiemba, Rashid Ismail, Abdallah Seseme, Haruna Chanongo na Mrisho Ngassa/Ramadhani Singano (dk. 73).

Coastal:- Shaaban Kado, Hamad Hamis, Abdi Banda, Mbwana Hamis/Castory Mumbara, Philip Mugenzi, Razak Khalfan, Daniel Lyanga, Mohamed Athumani, Deangelis da Silva/Mohamed Mtindi (dk.75), Selemani Kassim Salembe na Joseph Mahundi/Twaha Shekue (dk.46).


No comments:

Post a Comment