Tuesday, February 12, 2013

TASWA YAFUTA MDAHALO WA WAGOMBEA TFF


CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) kimefuta wazo la kuendesha mdahalo kwa wagombea wa nafasi za juu za uongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Taswa, Amir Mhando ilisema mdahalo huo ulikuwa ufanyike Februari 15, 2013 na tayari chama kilikuwa katika hatua nzuri ya mazungumzo na wadhamini pamoja na kituo kimoja cha televisheni kwa ajili ya kurusha 'live' tukio hilo, ambapo kesho ilikuwa watangaze utaratibu mzima wa mdahalo huo.

"Katika mazungumzo ya leo na uongozi wa kituo hicho ambao hatutaki tukitangaze, tumekubaliana kufuta wazo la mdahalo kwa  sababu nafasi ya urais amebaki mgombea mmoja, hivyo mdahalo hautakuwa na tija," alisema Mhando katika taarifa hiyo.

Alisema dhamira ya awali ya kufanya mdahalo ilikuwa kuwapa fursa wapiga kura wasikie vyema sera za wagombea urais na makamu wa rais ili wananchi wawasikilize wagombea hao na pia wapiga kura wawatambue vizuri.

"Hata hivyo TASWA itatafuta utaratibu mwingine mzuri ambao utawezesha wagombea kuzungumza na waandishi wa habari na kuulizwa maswali mbalimbali ambayo tunaamini kwa kiasi fulani yatasaidia wapiga kura katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Februari 24 mwaka huu. TASWA inawatakia kila la kheri wagombea wote wa TFF waliobakia," alisema katika taarifa hiyo.

TASWA imekuwa ikifanya mdahalo kwa wagombea wa nafasi za juu kwenye uchaguzi wa TFF ambapo ilifanya hivyo mwaka 2001 na mwaka 2004 ingawa haurushwa moja kwa moja lakini ikafanya wa 'live' mwaka 2008, ambapo yote ilikuwa ya mafanikio makubwa.

No comments:

Post a Comment