Wednesday, February 6, 2013

SABA WAPITISHWA KUWANIA UONGOZI TASMA


Mwanandi Mwankemwa
WATAALAMU saba wamepitishwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa Chama cha Wataalamu wa Tiba ya Michezo Tanzania (TASMA) utakaofanyika Februari 10 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TASMA, Dk. Paul Marealle, wagombea hao wamepitishwa baada ya kufaulu katika usaili uliofanyika jana (Februari 5 mwaka huu).

Mwenyekiti aliyemaliza muda wake Biyondho Ngome anatetea nafasi hiyo dhidi ya alikuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Mwanandi Mwankemwa. Nafasi ya Katibu Mkuu ina mgombea mmoja ambaye ni Nassoro Matuzya wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti haikupata mgombea.

Sheky Mngazija ni mgombea pekee wa nafasi ya Katibu Msaidizi kama ilivyo kwa Juma Mzimbiri aliyepitishwa kuwania nafasi ya Mhazini. Naye Hemed Mziray ni mgombea pekee wa nafasi ya ujumbe wa Kamati Kuu ya TASMA.

Nafasi ya Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemvutia Joakim Mshanga pekee.

Wapiga kura ni wajumbe sita wa Kamati ya Utendaji na wawakilishi watatu watatu kutoka mikoa ya Geita, Ilala, Iringa, Kagera, Kinondoni, Mtwara, Rukwa, Ruvuma na Temeke. Hivyo jumla ya wapiga kura wote ni 33.

No comments:

Post a Comment