Tuesday, February 26, 2013

KOCHA WA AZAM AFUNGIWA KWA KUVUA BUKTA NA KUBAKI NA KICHUPI UWANJANI, PIA ALIMWA FAINI YA SH. 500,000 NA TFF..!

Kocha Stewart Hall wa Azam akibebwa na wachezaji wake baada ya kutwaa Kombe la Mapinduzi visiwani Zanzibar.

Stewart Hall
Kocha wa Azam, Stewart John Hall amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya Sh. 500,000 kwa kwa kosa la kushusha bukta yake huku akimlalamikia refa msaidizi wakati wa mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya timu yake na Kagera Sugar iliyochezwa Januari 26 kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi jijini Dar es Salaam.

Adhabu hiyo imetolewa na Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana mwishoni mwa wiki kupitia ripoti za michuano ya VPL na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu wa 2012/2013 inayoendelea hivi sasa na kufanya uamuzi mbalimbali.

Naye Kocha Msaidizi wa timu ya Mgambo Shooting, Denis Mwingira ametozwa faini ya sh. 500,000 kwa kumtolea lugha chafu mwamuzi kwenye mechi dhidi ya Mtibwa Sugar iliyochezwa Oktoba mwaka jana katika Uwanja wa Manungu.

Ally Jangalu ambaye ni Kocha Msaidizi wa Polisi Morogoro naye ameangukiwa na rungu la Kamati ya Ligi kwa kupigwa faini ya sh. 500,000 baada ya kutolewa kwenye benchi kwa kupinga uamuzi wa refa kwa sauti ya juu. Alitenda kosa hilo kwenye mechi kati yao na Kagera Sugar iliyochezwa Novemba 10 mwaka jana Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

Matukio ya aina hiyo kwa kocha Jangalu yamekuwa ya kujirudiarudia ambapo Oktoba 13 mwaka jana katika mechi dhidi ya Azam iliyochezwa mjini Morogoro aliondolewa na mwamuzi kwenye benchi kwa kuchochea wachezaji wa timu yake wacheze rafu.

Naye Kocha wa timu ya Moro United inayoshiriki FDL, Yusuf Macho amepigwa faini ya sh. 200,000 kwa kumtolea lugha chafu refa baada ya mechi dhidi ya Transit Camp iliyofanyika Novemba 4 mwaka jana Uwanja wa Mabatini mjini Mlandizi.

Pia Kocha wa Burkina Faso, Hasheem Mkingie amepigwa faini ya Sh. 200,000 baada ya kutolewa kwenye benchi kwa kutoa lugha chafu katika mechi ya FDL dhidi ya Mkamba Rangers.

Kiongozi wa Majimaji, Joseph Nswila ambaye aliingia uwanjani baada ya mechi dhidi ya Mlale JKT kumalizika na kuvamia waamuzi amefungiwa miezi sita.

Vilevile timu ya Azam imepigwa faini ya sh. 300,000 kwa kuchelewa kufika uwanjani kwenye mechi kati yao na JKT Oljoro iliyochezwa Novemba 7 mwaka jana katika Uwanja wao wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam.

Pia Coastal Union imetozwa faini ya sh. 500,000 kutokana na washabiki wake kumrushia chupa za maji mwamuzi msaidizi namba mbili wakati wa mechi yao dhidi ya Simba iliyochezwa Oktoba mwaka jana Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Nayo klabu ya African Lyon imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa timu yake kugoma kuingia kwenye chumba cha kubadilishia nguo wakati wa mapumziko katika mechi dhidi ya Coastal Union iliyochezwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, Oktoba 24 mwaka jana.

Timu ya Burkina Faso ya Morogoro imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na kuonesha vitendo vya ushirikina kabla ya mechi yao dhidi ya Mbeya City iliyochezwa Oktoba 24 mwaka jana Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Faini ya ushirikina ya sh. 200,000 pia imepigwa timu ya Pamba baada ya kuonesha vitendo hivyo kwenye mechi yao dhidi ya Mwadui iliyochezwa Novemba 4 mwaka jana Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.

Nayo Mkamba Rangers imepigwa faini ya sh. 200,000 baada ya washabiki wake kumtolea lugha chafu Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Morogoro (MRFA), Hamis Semka na kumrushia chupa za maji mwamuzi wa mezani katika mechi dhidi ya Mbeya City iliyochezwa mjini Morogoro.

Polisi Dodoma imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na washabiki wake kuvamia uwanjani na kutaka kuwapiga waamuzi katika mechi yao dhidi ya JKT Kanembwa na kusababisha mipira miwili ya Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dodoma (DOREFA) kupotea.

Pia klabu kadhaa zimeandikiwa barua za onyo kwa timu zao kuchelewa kufika uwanjani au kutofika kwenye mkutano wa maandalizi ya mechi (Pre-match meeting). Klabu hizo ni Coastal Union, JKT Ruvu, Toto Africans, Simba, Green Warriors, Majimaji, Mkamba Rangers, Polisi Dodoma, JKT Kanembwa, Moro United.

Mchezaji Stanley Nkomola wa JKT Ruvu baada ya mechi dhidi ya Coastal Union alikwenda jukwaani na kuanza kupigana na washabiki. Pia kipa wa timu ya Transit Camp, Baltazar Makene baada ya mechi dhidi ya Tessema aliruka uzio na kwenda kupigana na washabiki.

Kwa vile masuala ya wachezaji hao ni ya kinidhamu yamepelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu inayoongozwa na Kamishna wa Polisi (CP) mstaafu Alfred Tibaigana kwa ajili ya kuchukuliwa hatua.

TFF KUJADILI TAMKO LA SERIKALI
Sekretarieti ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imepokea barua ya Serikali ikielezea uamuzi wa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara kutengua uamuzi wa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo nchini kuidhinisha marekebisho ya Katiba ya TFF toleo la 2012.

Baada ya kupokea barua hiyo jana alasiri (Februari 25 mwaka huu), Sekretarieti iliwasiliana na Rais wa TFF, Leodegar Tenga ambaye ameagiza kuitishwa kikao cha dharura cha Kamati ya Utendaji kujadili tamko hilo.

Kikao hicho cha Kamati ya Utendaji ya TFF kitafanyika Jumamosi (Machi 2 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment