Thursday, January 10, 2013

MOURINHO KOCHA BORA WA KLABU 2012

KOCHA Mreno Jose Mourinho, wa Real Madrid, ameshinda tuzo ya Kocha Bora wa Klabu 2012 zilitolewa na Shirikisho la Kimataifa la Historia na Takwimu za Soka (IFFHS). Hii ni mara ya nne anatwaa tuzo hiyo.

Katika kura ambazo hupigwa na maafisa wa IFFHS na wataalamu, Mourinho, ambaye ametwaa ubingwa Ligi Kuu ya Hispania na Kombe la "Super Cup", alimpiku Muitalia Roberto Di Matteo, ambaye aliiongoza Chelsea kutwaa ubingwa wa Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya na Kombe la FA.

Mourinho, ambaye alitwaa tuzo hiyo mwaka 2004, 2005 na 2010, alivunja rekodi ya pointi na magoli katika La Liga akiwa na timu yake ya Real Madrid na akatolewa kwa matuta katika nusu fainali ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya dhidi ya Bayern Munich.

Makocha wengine waliopata kutwaa tuzo hiyo kwa zaidi ya mara moja ni Marcello Lippi (1996 na 1998), Ottmar Hitzfeld (1997 na 2001), Carlos Bianchi (2000 na 2003), Sir Alex Ferguson (1999 na 2008) na Pep Guardiola (2009 na 2011).

Mshindi wa tatu wa tuzo hiyo 2012, Diego Pablo Simeone, alishinda ubingwa wa Ligi ya Europa na UEFA Super Cup akiwa na Atletico Madrid, ambayo hivi sasa ni ya pili katika msimamo wa La Liga nyuma ya Barcelona. Kocha huyo Muargentina alimshinda Pep Guardiola, ambaye anachukua mapumziko ya mwaka mmoja, baada ya kutwaa ubingwa wa Kombe la Mfalme akiwa na Barcelona 2012.

No comments:

Post a Comment