Saturday, December 15, 2012

WARAKA WA MAREKEBISHO YA KATIBA YA TFF WAPITA


Waraka wa marekebisho ya Katiba ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) umepita baada ya kuungwa mkono na theluthi mbili ya wajumbe wa Mkutano Mkuu waliopiga kura.

Jumla ya wajumbe waliopiga kura kwa njia hiyo ya waraka ni 103 ambapo 70 wameunga mkono wakati waliokataa ni 33. Idadi hiyo ni asilimia 68 ya kura zote zilizopigwa, hivyo kupatikana theluthi mbili ya kura zilizopigwa ili kufanya marekebisho kikatiba.

Kura zilizosema ndiyo kutoka kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa vyama vya mikoa ni 46, wajumbe kutoka vyama shiriki ni 13 wakati klabu za Ligi Kuu zilizounga mkono ni kumi na moja.

Kamati ya Utendaji ya TFF inawashukuru wajumbe wote wa Mkutano Mkuu- kwa waliounga mkono na waliokataa kwa vile walikuwa wanatekeleza wajibu wao wa kikatiba.

Vipengele vilivyoingizwa ni ‘club licencing’ kama ilivyoagizwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Kamati ya Rufani ya Uchaguzi wa TFF kama ilivyoshauriwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) na kuondoa nafasi ya Makamu wa Pili wa Rais.

Vilevile Kamati ya Utendaji itakutana Desemba 23 mwaka huu kufanya marekebisho ya Kanuni za Uchaguzi, kutokana na kupitishwa kwa marekebisho hayo ambayo yanaunda Kamati ya Rufani ya Uchaguzi wa TFF. Pia itachagua wajumbe wa Kamati ya Rufani ya TFF.

Mkutano Mkuu wa TFF ambapo pia utakuwa na ajenda ya uchaguzi utafanyika Februari 23 na 24 mwakani. Kwa mujibu wa Katiba ya TFF, wajumbe wanatakiwa kupewa taarifa ya Mkutano Mkuu siku 60 kabla.

No comments:

Post a Comment