Friday, December 14, 2012

MTIBWA SUGAR YAICHAPA TOTO 3-1 KOMBE LA UHAI


Mtibwa Sugar ya Morogoro leo asubuhi (Desemba 14 mwaka huu) imeibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Toto Africans ya Mwanza katika mechi ya michuano ya Kombe la Uhai inayoshirikisha timu za vijana wenye umri chini ya miaka 20 (U20) za klabu za Ligi Kuu ya Vodacom.

Juma Luzio alifunga mabao yote matatu (hat trick) katika mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam. Alifunga mabao hayo dakika za 44,81 na 88.

Hata hivyo, Toto Africans ndiyo walioanza kufunga katika mechi hiyo ya kundi A. Bao hilo katika michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia maji Uhai lilifungwa dakjika ya 22 na Pastol Makula.

Nayo Simba imenguruma baada ya kuitandika Mgambo Shooting ya Tanga katika mechi nyingine ya michuano hiyo iliyochezwa leo asubuhi kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi. Wafungaji kwa washindi walikuwa Ramadhan Mdoe dakika ya 19, Mohamed Salum dakika ya 77 na Ramadhan Singano dakika ya 89.

Michuano hiyo inaendelea leo mchana na jioni. Mechi ya Ruvu Shooting na Kagera Sugar iliyokuwa ichezwe mchana Uwanja wa Azam, Chamazi sasa itafanyika saa 10 kamili jioni katika Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume.

Mechi nyingine za leo ni Coastal Union vs JKT Ruvu (mchana- Karume), African Lyon vs Azam (jioni- Chamazi). Vilevile mechi kati ya JKT Oljoro na Yanga inachezwa leo Uwanja wa Chamazi.

Kesho (Desemba 15 mwaka huu) ni mapumziko, na michuano hiyo itaendelea Jumapili kwenye viwanja vyote viwili- Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume na Uwanja wa Azam- Chamazi.

No comments:

Post a Comment