Tuesday, December 11, 2012

AZAM WAMWAGA MAMILIONI KUKAMILISHA USAJILI WA MGANDA BRIAN UMONY… NI STRAIKA BORA ALIYEISAIDIA TAIFA UGANDA KUTWAA KOMBE LA CHALENJI ... ALIFUNIKA MBAYA NA KUTWAA TUZO YA MWANASOKA BORA WA MICHUANO HIYO…!


Umony (mbele) akimuacha mtu wakati wa michuano ya Chalenji iliyoisha Jumamosi.


KLABU ya Azam imezidi kujiimarisha baada ya kumsajili straika wa kimataifa wa Uganda, Brian Umony kwa dau lisilotajwa lakini linalodaiwa kuwa ni la ‘hela ndefu’ ya mamilioni ya fedha, imefahamika.

Taarifa zilizothibitishwa leo na Meneja wa Azam, Patrick Kahemele, zimeeleza kwamba straika huyo bora wa Uganda ‘aliyefunika’ ile mbaya katika michuano iliyomalizika hivi karibuni ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Chalenji) na kutwaa Tuzo ya Mchezaji Bora wa Chalenji 2012, ameshamalizana na waajiri wake wapya na kusaini mkataba wa miaka miwili.

Ataichezea timu hiyo katika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Akizungumza leo kutokea Kampala, Meneja wa Azam, Patrick Kahemele, alisema kuwa tayari wameshamalizana na Umony na mchezaji huyo atatua jijini Dar es Salaam kesho kujiunga na wachezaji wenzake walio kambini kujiandaa na ziara yao ya Kinshasa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

“Kila kitu kimeshakamilika, tumeshaingia naye (Umony) mkataba wa miaka miwili na kesho kutwa  atapanda ndege hapa Kampala kuja huko (Dar es Salaam) kuungana na wachezaji wenzake wa Azam,” amesema Kahemele, ambaye hata hivyo hakuwa tayari kutaja ada ya uhamisho waliyotumia kumpata mchezaji huyo wala maslahi yake.

Afisa Habari wa Azam, Jaffer Idd Maganga, alisema kikosi chao kitaondoka jijini Dar es Salaam Ijumaa kuelekea Kinshasa ambako kitaweka kambi kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Klabu ya El Merreikh ya Sudan iliyomnasa Mrisho Ngassa, nayo ilituma mwakilishi wake kwenda kuzungumza na Umony wiki iliyopita, lakini nayo ikashindwa dhidi ya mikakati ya Azam ambayo itawakilisha Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika inayoandaliwa na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF).

Umony aling’ara katika michuano ya Kombe la Chalenji iliyomalizika Jumamosi jijini Kampala, Uganda na kuibuka Mchezaji Bora wa michuano hiyo mwaka huu baada ya kuonyesha kiwango safi na kufunga magoli matatu yaliyoisaidia Ugandae kutwaa ubingwa.
 
Alirejea Uganda na kujiunga na KCC baada ya kumaliza mkataba wake na klabu ya Becamex Binh Duong ya Vietnam. Aliwahi pia kuzichezea klabu za SuperSport United ya Afrika Kusini, klabu ya Chuo Kikuu cha Pretoria ya Afrika Kusini na pia akaichezea kwa mkopo wa mwaka mmoja klabu ya Portland Timbers ya Marekani.



No comments:

Post a Comment