Thursday, November 1, 2012

TAZAMA SHEIKH PONDA NA WAISLAMU WENGINE 49 WALIVYOFIKISHWA MAHAKAMA YA KISUTU LEO HUKU WAKILINDWA NA UTIRIRI WA ASKARI POLISI WA KAWAIDA, FFU NA MAGEREZA … WAMWAGWA PIA ASKARI WENYE SILAHA, MAGARI KIBAO, FARASI, MBWA TELE… WATU WAKAGULIWA KORTINI KWA MITAMBO MAALUM YA CCTV… PINGAMIZI LA MKURUGENZI WA MASHTAKA (DPP) KUPINGA DHAMANA YA SHEIKH PONDA LAENDELEA HIVYO PONDA NA WENGINE 49 WARUDISHWA RUMANDE HADI KESI ITAKAPOTAJWA TENA ALHAMISI NOV. 15


Sheikh Ponda akifunguliwa pingu kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Alhamisi, Novemba 1, 2012. 
Askari wa kikosi cha farasi wakizuia waumini wa dini ya Kiislamu waliofika mahakamani kuhuhudhuria  kesi ya Sheikh Ponda leo Alhamisi Novemba 1, 2012.

Sheikh Ponda na wenzake wakiongozwa kutoka ndani ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Novemba 1, 2012.

 

Sheikh Ponda akiwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Novemba 1, 2012.


Baadhi ya Waislamu walioshtakiwa pamoja na Sheikh Ponda wakifunguliwa pingu kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Alhamisi Novemba 1, 2012.
Mshtakiwa mmojawapo miongoni mwa Waislamu 49 walioshtakiwa pamoja na Sheikh Ponda akiwa amebebwa na mwenzake baada ya kudondoka mahakamani na kupoteza fahamu leo Alhamisi Novemba 1, 2012.


Mmoja wa maaskari tele waliomwagwa kwenye Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam leo akiendelea na lindo lake wakati wa kutajwa kwa kesi ya Sheikh Ponda na Waislamu wengine 49 leoAlhamisi Novemba 1, 2012
Polisi wa kikosi cha mbwa pia walimwagwa kwenye Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam leo wakati wa kutajwa kwa keshi ya Sheikh Ponda na Waislamu wengine 49.
Ukaguzi wa kila mtu kwa vifaa maalum ukiendelea kwenye geti la kuingilia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Alhamisi, Novemba 1, 2012.

Polisi wa Mbwa wakisubiri amri ndani ya gari lao nje ya mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam, leo Alhamisi Novemba 1, 2012
Polisi wa Mbwa akifanya doria kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo Novemba 1, 2012 wakati wa kutajwa kwa kesi ya Sheikh Ponda.



Utitiri wa askari polisi wa kawaida, FFU, Magereza na wengine wa upelelezi waliovalia kiraia walimwagwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo wakati wa kutajwa kwa kesi inayomkabili Sheikh Ponda Issa Ponda na Waislamu wengine 49.

Katika eneo la mahakama kulikuwa pia na utitiri wa mbwa, farasi na magari yaliyosheheni askari zaidi kwa nia ya kuimarisha usalama.

Ponda na wenzake wanakabiliwa na mashitaka matano ambayo ni pamoja na kula njama, kuingia, kujimilikisha ardhi kwa jinai na wizi wa mali ya Sh. milioni 59.6.  Sheikh Ponda pia anakabiliwa na shitaka la uchochezi.

Watu waliokuwa wakipita kwenye lango la kuingilia mahakamani hapo walikuwa wakikaguliwa kila mmoja kwa mitambo maalum.

Kuanzia mishale ya saa 2:00 asubuhi,   askari zaidi wenye sare za polisi na magereza waliomgezeka eneo la mahakama huku wakiwa na silaha na zana mbalimbali za kukabiliana na tishio lolote la uvunjifu wa amani.

Wakati wa kutajwa kwa kesi hiyo, Hakimu Mkazi, Victoria Nonga, aliwasomea washtakiwa 49 masharti ya dhamana isipokuwa Sheikh Ponda ambaye ni mshtakiwa namba moja kwa maelezo kwamba Mkurugenzi wa Mashtaka Tanzania (DPP) ameendelea kuweka pingamizi kuzuia dhamana yake.

Washtakiwa wengine walitakiwa kuwa na mdhamini mmoja kila mmoja atakayesaini hati ya dhamana ya Sh. milioni moja na kila mmoja angeachiwa kama angetimiza masharti hayo. Hata hivyo, wote walirejeshwa rumande pamoja na Sheikh Ponda baada ya kile kilichoelezwa kuwa ni kutotimiza masharti waliyopewa. Kesi hiyo itatajwa tena Alhamisi ya Novemba 15.

Awali, wakili mwandamizi wa serikali, Tumaini Kweka, alidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kuiomba Mahakama kupanga tarehe ya kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali.

Sheikh Ponda na wenzake 49 walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Oktoba 18 mwaka huu na kusomewa mashtaka kabla DPP kuwasilisha hati ya kiapo cha kupinga dhamana ya Sheikh Ponda kwa maslahi ya taifa.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Seleman Wajumbe, Salum Juma, Salum Mkwasu, Ramha Hamza, Halima Abas, Maua Mdumila,  Fatihiya Habibu, Hussein Ally na Kurthum Mohamed,  Zaldah Yusuph, Juma Mpanga,  Farida Lukoko,  Adamu Makilika na Athumani Salim.

Wengine ni Alawi Alawi, Ramadhani Mlali,  Omary Ismaili, Salma Abduratifu,  Khalidi Abdallah,  Said Rashid, Shaban Ramadhani, Hamis Mohamed, Rashid Ramadhani, Yusuph Penza,  Feswali Bakari,  Issa Wahabu, Ally Mohamed,  Abdallah Senza, Juma Hassani,  Mwanaomary Makuka na Mohamed Ramadhani.

Wengine ni Smalehes Mdulidi, Jumanne Mussa, Salum Mohamed, Hamis Halidi, Dite Bilali, Omary Bakari,  Maulid Namdeka,  Farahan Jamal,  Amiri Said, Juma Yassin, Rashid Ndimbu,  Hamza Ramadhani, Ayubu Juma, Athuman Rashid, Rukia Yusuph, Abubakar Juma na Ally Salehe.

Awali, upande wa mashtaka ulidai kuwa katika shtaka la kwanza, Oktoba 12, 2012,  katika eneo la huko Temeke jijini Dar es Salaam, Sheikh Ponda na wenzake walikula njama ya kutenda makosa.

Shitaka la pili linadai kuwa siku ya tukio la kwanza, eneo la Chang’ombe Markas, Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam, washtakiwa hao kwa jinai walivamia kwa nia ya kutaka kujimilikisha kiwanja ambacho ambacho ni mali ya kampuni ya Agritanza.

Katika shitaka la tatu, imedaiwa kuwa kati ya Oktoba 12 na 16, 2012, katika eneo la Chang’ombe Markas, pasipo uhalali, washtakiwa walijimilikisha ardhi hiyo.

Katika shtaka la nne, imedaiwa kuwa kati ya Oktoba 12 na 16, mwaka huu, karika eneo hilo, washtakiwa waliiba vifaa mbalimbali vya ujenzi yakiwamo matofali 1,500, tani 36 za kokoto na nondo vyenye thamani ya Sh. 59,650,000.

Shtaka la tano lililodaiwa ni Jamhuri ni kuwa, kati ya Oktoba 12 na 16 mwaka huu, eneo la Chang’ombe Markas, Sheikh Ponda akiwa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, aliwashawishi wafuasi wake kutenda makosa ya jinai. Washtakiwa wote wamekana mashtaka.

Eneo la Markas lililomponza Sheikh Ponda na Waislamu wengine 49 waliokuwa wameweka kambi eneo hilo lilikuwa likimilikiwa na Waislamu kupitia Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kwa ajili ya shughuli mbalimbali zikiwamo za kujengea chuo kikuu, lakini inadaiwa kuwa baadaye likauzwa.

No comments:

Post a Comment