Thursday, November 29, 2012

LIONEL MESSI, CRISTIANO RONALDO NA ANDRES INIESTA WATINGA 3-BORA YA WANAOWANIA TUZO YA MWANASOKA BORA WA MWAKA WA DUNIA -- FIFA BALLON D'OR... MSHINDI KUTANGAZWA JAN 7… DEL BOSQUE, JOSE MOURINHO NA PEP GUARDIOLA KUCHUANA TUZO YA KOCHA BORA FIFA

Lionel Messi

Cristiano Ronaldo

Andres Iniesta


Vicente Del Bosque
Jose Mourinho
Pep Guardiola
RIO DE JANEIRO, Brazil
Nyota wa Barcelona, Lionel Messi na Andres Iniesta na wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo walitangazwa kuwamo katika orodha ya wachezaji watatu watakaochuana kuwania Tuzo ya Mwanasoka Bora wa FIFA (FIFA Ballon d'Or) katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika leo nchini Brazil.

Muargentina Messi ameshinda tuzo hiyo, zamani ikijulikana kama Tuzo ya Mwanasoka Bora wa Mwaka wa Dunia, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita na sasa anapewa nafasi kubwa ya kushinda tena baada ya kuendelea na kasi yake ya kufunga magoli ‘atakavyo’.

Messi na Ronaldo ambaye pia hufunga magoli kama mvua, mara kwa mara wamekuwa wakibishaniwa kuwa ni nani mkali zaidi ya mwingine kati yao na mwaka huu hauna tofauti kwani wanaonekana kuchuana vikali zaidi katika kila wiki.

Kocha wa Ronaldo katika klabu ya Real Madrid, Jose Mourinho, alisema hivi karibuni kwamba itakuwa ni kosa la jinai ikiwa mchezaji wake hatashinda Tuzo ya Ballon d'Or kwa mara ya pili, ikiwa ni baada ya maoni kutoka kwa kocha wa Barcelona,  Tito Vilanova aliyemuelezea Messi kama "mchezaji mkali kuliko wote duniani, kwa tofauti kubwa kulinganisha na wengine ".

"Kama Messi ndiye bora zaidi duniani, Ronaldo ni bora zaidi ulimwenguni. Itakuwa ni kosa la jinai ikiwa Ronaldo hatashinda Tuzo ya Ballon d'Or," Mourinho alisema Oktoba, muda mfupi baada ya mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Ureno kuwa mchezaji wa kwanza kuwahi kufunga magoli katika mechi sita mfululizo za 'Clasico', ambazo huwakutanisha mahasimu wa jadi Barcelona na Real Madrid.

Messi alifunga magoli 50 katika La Liga, Ligi Kuu ya Hispania msimu uliopita, manne zaidi ya Ronaldo, na ameshafunga magoli 82 katika mwaka wa kalenda hadi sasa, yakibaki magoli matatu kabla ya kuifikia rekodi ya magoli 85 iliyowekwa na Gerd Mueller mwaka 1972.
Hata hivyo, Ronaldo ambaye ni mshindi wa tuzo hiyo mwaka 2008 alikuwa mhimili wa Real Madrid katika safari yake ya kutwaa taji la Ligi Kuu ya Hispania msimu uliopita na pia  kuisaidia Ureno kufika nusu fainali ya michuano ya Euro.

Iniesta ndiye mchezaji pekee kati yao aliyetwaa taji la Kombe la Dunia na mataji mawili ya Euro akiwa na timu yake ya taifa ya Hispania.

Kama Messi atashinda tuzo hiyo mjini Zurich Januari 7, atakuwa mwanasoka wa kwanza kushinda tuzo hiyo mara nne mfululizo.

Wanaowania Tuzo ya Kocha Bora wa Mwaka wa Dunia ni kocha wa timu ya taifa ya Hispania, Vicente del Bosque, kocha wa zamani wa Barcelona, Pep Guardiola na Mourinho.

Alex Morgan na Abby Wambach wa timu ya taifa ya Marekani  na Mbrazil Martha wametajwa katika orodha ya nyota watatu watakaowania Tuzo ya FIFA ya Mwanasoka Bora Mwanamke wa Mwaka wa Dunia.

Uteuzi huo umetokana na kura ambazo zimepigwa na manahodha na makocha wa timu za taifa za soka za wanaume na wanawake, pamoja na vyombo vya habari teule.




No comments:

Post a Comment