Sunday, October 21, 2012

SOFIA SIMBA ASHINDA TENA UENYEKITI UWT … AMGARAGAZA VIBAYA ANNE KILANGO MALECELA ALIYEKUWA AKISINDIKIZWA NA MZEE MALECELA NA KUPIGWA BUSU KALI HADHARANI… KABLA YA KUIBUKA MSHINDI SOPHIA SIMBA NUSRA ATWANGANE MAKONDE UKUMBINI NA SHYROSE-BHANJI... DK. NAGU AWATULIZA!


Sofia Simba akishangilia baada ya kujua kuwa 'amemgaragaza' vibaya mpinzani wake Anne Kilango Malecela katika uchaguzi wa Mwenyekiti wa UWT mjini Dodoma.

Mjumbe wa NEC -CCM mkoa wa Manyara, Dk. Mary Nagu (kulia) akijaribu kumtuliza Shy-Rose Bhanji aliyekuwa akikaribia kuchapana na Sofia Simba wakati wa uchaguzi wa Mwenyekiti wa UWT taifa mjini Dodoma. .
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT), Sophia Simba, ameibuka kidedea ambapo ametetea kiti chake kwa kumbwaga mpinzani wake mkubwa Anna Kilango Malecela kwa zaidi ya nusu ya kura zilizopigwa katika Uchaguzi Mkuu wa jumuiya hiyo uliofanyika jana mjini hapa.
Akitangaza matokeo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi huo, Abdulhamani Kinana, alimtangaza Simba, ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kuwa mshindi wa kiti hicho.


Jumla ya kura zilizopigwa katika uchaguzi huo zilikuwa 1,038 na mbili kati ya hizo ziliharibika ambapo Simba alizoa kura zaidi ya 700 huku mpinzani wake akipata kura zaidi ya 300 na nafasi ya mwisho ikishikiliwa na  MayRose Majinge, aliyeambulia kura saba.


Awali uchaguzi huo ulitawaliwa na mizengwe baada ya Simba na Mbunge wa Afrika Mashariki,  Shyrose Banji, kutaka kuchapana makonde. 


Aidha, posho za wajumbe kutoka mkoa wa Pwani zilitangazwa kuibiwa katika mkutano huo.
Hali hiyo ilitokea muda mfupi jana baada ya Simba kujibu swali lililoulizwa na Bhanji, akimtaka aeleze wapiga kura atawezaje kukivusha chama katika uchaguzi mkuu ujao ikiwa haonekani katika majukwaa ya siasa kuhamasisha wanawake kujiunga na umoja huo. 


Hata hivyo, Bhanji alipata wakati mgumu baada ya kukatishwa mara kwa mara na kelele za wajumbe walionekana kukerwa na swali lake. 


Akijibu swali hilo Simba ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, alisema Bhanji hajui siasa za chini kwa chini. 


Alisema yeye ni serikali kwa hiyo hawezi kuikosoa serikali bungeni,” Siwezi kukikosoa chama changu bungeni. Wabunge wa CCM hawatakiwi kukikosoa chama chako kwa mithili ya kukiangusha.” 


Alisema mwaka 2010 walihangaika yeye na Baraza lake kupita nchi nzima kuomba kura kwa wananchi na kwamba Rais Jakaya Kikwete alikiri kuwa ushindi huo umeletwa na wanawake. 


“Mimi ndio kamanda wenu nichagueni mimi…. Huyu amepata ubunge wa Afrika Mashariki hivi karibuni hajui huko chini mmefanya nini CCM,” alisema na kushangiliwa na wajumbe. 


Baada ya kumalizika kwa Swali hilo, Mwenyekiti wa mkutano huo ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna  Tibaijuka,  alimtaka kwenda kuchukua nafasi yake na hapo ndipo wapambe wa Simba kutoka  Mkoa wa Dar es Salaam walipomtaka Bhanji aliyekaa katika kiti cha mgombea huyo kuondoka. 


Hata hivyo, alipofika katika eneo hilo, Simba alimtupia kijembe Bhanji, “ huniwezi wewe’ hali iliyomfanya Bhanji kuhamaki na kutaka kusikia tena “what” ( nini). 


Kutokana na kuhamaki huko,  baadhi ya wajumbe waliinuka na kwenda kuamulia kwa kumshawishi Bhanji kutoka katika eneo hilo kwa ajili ya usalama. 


Aidha, katika mkutano huo, Mshereheshaji ambaye ni Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Pwani, Zainabu Vullu, alitangaza kuibiwa kwa posho za wajumbe wa mkutano wa mkoa wa Pwani zaidi ya 40. 


“Waheshimiwa wajumbe kuna mtu amechukua mkoba ambao si wake, ulikuwa na posho za wajumbe naomba jamani aliyechukua arudishe ili wenzenu waweze kupata posho,”alisema. 


Awali kabla ya kuanza kujieleza kwa wagombea wa nafasi hiyo,  Profesa Tibaijuka,  alitaka kuanza kujieleza kwa wagombea  hao, ambapo alianza kuja majina ya wagombea watatu. 


“Ataanza MayRose Majinge, Anne Malecela Kilango na kufuatiwa na Sophia Simba ambaye mambo yake tumeshayaona hapa,”alisema.


MAJINGE
Alisema kuvaa khanga na kuimba nyimbo sio kigezo cha kumchagua mgombea bali wanatakiwa waangalie maendeleo.
“Mimi ninatosha katika maarifa, taaluma na kimaadili, nitumeni mimi nikawatumikie,” alisema.

MALECELA
Malecela ambaye awali alisindikizwa na mumewe, Mzee John Malecela hadi mlangoni ambapo alimbusu kama ishara ya kumtakia uchaguzi mwema, aliingia katika eneo la kipaza sauti akiwa ameshikilia biblia yake mkononi. 


Alisema uchaguzi wa mwaka 2015 utakuwa mgumu hivyo kunahitajika kiongozi  madhubuti atakayeweza kuivusha CCM katika uchaguzi huo. 


Alisema uwezo wa kukijenga chama anao na uwezo wa kukivusha chama katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. 


Pia alisema anaumia sana na suala la watendaji wa chama hicho kutenganishwa kikazi na wenza wao, jambo ambalo linawafanya ndoa zao kuwa mashakani. 


Alisema kuwa  kwa kusaidiana na wenzake, atatafuta njia ya kuwawezesha watendaji hao kuishi katika eneo moja.

SOPHIA SIMBA
Alisema ukomo ulioamuliwa ulikuwa ni kwa upande wa ubunge wa viti maalum tu na wala si kwa madiwani.
Alisema suala hilo litaamuliwa  na wanawake wa CCM na wale walio nje ya chama hicho katika utungaji wa katiba mpya. 


Pia alisema umoja huo uko mbioni kujenga jengo la ghorofa 16 ambalo litajulikana kama Mama Nyerere Tower. 


Dk. GHALIB MOHAMMED BILAL
Awali akifungua mkutano, Makamu wa Rais, Dk Gharib Mohammed Bilal, aliwataka wajumbe hao kutochagua viongozi waliojaa rushwa na wale wanaonunua uongozi. 


“Uongozi ni utumishi sasa wale wanaonunua maana hawataki kuja kututumikia. Ni marufuku kabisa kwenu na chama kwa ujumla kuwa nyinyi ni madalali wa rushwa,” alisema na kuongeza:
“Hao wanaowanunua muwaulize wamegundua mtaji gani huko? Kwa hiyo yeyote mnaedhania tu kuwa katumia rushwa msimpe uongozi.”

HALI KABLA YA MKUTANO
Katika nje ya ukumbi wa Chuo cha Mipango mjini hapa, kulikuwa na makundi mawili yaliyokuwa yakirushiana tambo na vijembe vya kila aina kwa wapambe wa wagombea wawili (Simba na Malecela).
Wapambe wa Malecela walisikika wakiimba kuwa wanataka mabadiliko huku wale wa Simba wakisema hawataki mabadiliko. 


Mgombea wa kwanza kuwasili katika viyunga vya ukumbi huo, alikuwa Simba ambaye alisimama getini akiomba kura kutoka kwa wajumbe wa mkutano huo, huku Majinge akionekana akifuata mjumbe mmoja mmoja mahali alipoketi. 


Hali ilikuwa sawa kwa Malecela aliyekuwa pia akiwafuata wajumbe walipokaa na kuowaomba kura.

RUSHWA
Taasisi ya Kuzuia Rushwa (Takukuru), walipiga kambi katika vyoo vya ukumbi huo wa mkutano ili kudhibiti rushwa. 


“Kila saa mnaingia chooni na kurudi, tupo hapa tunawaangalia,”alisikika mmoja wa  watu wanaodhaniwa kuwa ni maofisa wa Takukuru.
Chanzo: Nipashe Jumapili 



No comments:

Post a Comment