Friday, October 5, 2012

SAMUEL ETO'O KIBOKO... APIGA 2 KUIPA ANZHI USHINDI WA 2-0 LIGI YA EUROPA... MABINGWA ATLETICO MADRID SAFI, LIVERPOOL ALIYEWAROGA KWELI KAFA... WACHAPWA 3-2

Samuel Eto'o Fils
Samuel Eto'o wa Anzi akianza kumuacha beki wa wapinzani wao kwa kasi ya umeme.
BERNE, Uswisi
SAMUEL Eto'o alifunga mara mbili na kuipa Anzhi Makhachkala ushindi wa 2-0 wa Ligi ya Europa League dhidi ya Young Boys jana wakati Liverpool walilala 3-2 nyumbani dhidi ya Udinese huku Videton, Sparta Prague na Molde zikipata ushindi usiotarajiwa.

Mabingwa watetezi Atletico Madrid, moja ya timu zilizochezesha vikosi vya pili, walihitaji goli la dakika za dakika za majeruhi kutoka kwa Cristian Rodriguez kuilaza Viktoria Plzen ya Czech 1-0.

Mchezaji huyo wa Uruguay anayefahamika kama "Kitunguu" alipiga shuti la kutokea nje ya boksi kuipa timu hiyo inayofundishwa na Diego Simeone pointi sita kutokana na mechi mbili kileleni mwa Kundi B.

Eto'o, ambaye wiki iliyopita alimaliza tofauti zake na maafisa wa Cameroon na kukubali kurejea kuichezea timu yao ya taifa tena, alifunga penalti ya dakika ya 62 iliyowapa goli la kuongoza kinyume na ulivyokuwa mwelekea wa mechi.

Kisha akaunganisha krosi ya Oleg Shatov katika dakika ya mwisho na kukamilisha ushindi wa 2-0 dhidi ya Waswisi hao na kuongeza mwendo wa bila ya kupoteza mechi ya Anzhi kufikia mechi sita katika michuano hiyo, zikiwamo za kuwania kufuzu.

Mechi hiyo ya Kundi A ilichezwa mbele ya mashabiki wachache mjini Moscow, ambako Anzhi wanachezea kutokana na sababu za kiusalama baada ya UEFA kukataa kuwaruhusu kuchezea mechi zao katika eneo lililojaa uhalifu la Dagestan.

Liverpool ilikuwa timu nyingine iliyowapumzisha nyota wa kikosi cha kwanza lakini bado waliongoza wakati wa mapumziko kupitia kwa Jonjo Shelvey.

Hata hivyo, Antonio Di Natale alisawazisha kwa goli lililofungwa kiufundi baada ya mapumziko na kisha akapika kwa werevu goli la tatu lililofungwa na Giovanni Pasquale muda mfupi baada ya beki wa Liverpool, Sebastian Coates kujifunga kwa kichwa.

Liverpool wakamuingiza mshambuliaji wa Uruguay, Luis Suarez ambaye alifunga kwa 'fri-kiki' ya hatari iliyokwenda moha kwa moja wavuni lakini hakuweza kusaidia kupata goli la kusawazidha.

Videoton walilipa soka la Hungary "boost" kwa ushindi wa 3-0 dhidi ya Sporting, magoli yakija katika kipindi cha kwanza kutoka kwa Paulo Vinicius, Filipe Oliveira na Nemanja Nikolic, wakati Sparta Prague waliwafunga washindi wa pili wa msimu uliopita Athletic Bilbao 3-1.

Molde, inayofundishwa na straika wa zamani wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer waliifunga VfB Stuttgart ya Ujerumani 2-0 kwa magoli ya kipindi cha pili kutoka kwa Jo Inge Berget na Daniel Chima.

Inter Milan walifurahia ushindi mwepesi wa 3-1 ugenini Azerbaijan dhidi ya Neftci thanks kwa magoli ya kipindi cha kwanza ya Philippe Coutinho, Joel Obi na Marko Livaja, yote yakipikwa na Mcolombia Fredy Guarin.

Waitalia wenzao Lazio walilazimisha ushindi wa 1-0 nyumbani dhidi ya klabu ya Slovenia ya Maribor kwa goli la dakika ya 62 la Mbrazili Ederson. Walipanda mpka kileleni mwa Kundi J wakiwa na pointi 4.

Tottenham Hotspur bado wanasubiri ushindi wao wa kwanza baada ya kutoka sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Panathinaikos.

Napoli, timu nyingine iliyopumzisha "majembe" yake huku Edinson Cavani akiwa mmoja wao waliokaa benchi, walikuwa timu pekee walioiangusha Italia baada ya kupigwa na timu ya kocha Dick Advocaat ya PSV kupitia magoli ya Jeremain Lens, Dries Martins na Marcelo waliofunga moja kila mmoja katika kipigo cha 3-0.

Timu ya Twente Enschede ya kocha wa zamani wa timu ya taifa ya England, Steve McClaren iliiponea kipigo kwenye tundu ya sindano ugenini Helsingborg baada ya Rasmus Bengtsson na Douglas kusawazisha na kuwapa sare ya 2-2. Magoli mawili kutoka kwa Nicola Djurdic yaliwaweka Wasweden mbele 2-0 wakati wa mapumziko.

Olympique Marseille walifunga mara nne katika nusu saa ya mwisho wa mechi wakati walipozinduka kutoka nyuma na kuisambaratisha AEL Limassol kwa magoli 5-1 huku Wafaransa wenzao Olympique Lyon, wakipoteza uongozi wao wa 3-1, kabla ya kushinda 4-3 ugenini dhidi ya mabingwa wa Israeli, Hapoel Kiryat Shmona.

No comments:

Post a Comment