Waziri Mkuu Pinda (kushoto), Nadir Haroub 'Cannavaro' (katikati) na mama Fatuma Karume wakifurahia Kombe la Yanga nje ya bunge mjini Dodoma |
Wachezaji wa Yanga wakipozi kwa picha pamoja na Waziri Mkuu Pinda, kocha wao Tom Saintfiet na mama Fatuma Karume nje ya ukumbi wa Bunge mjini Dodoma. |
Mbunge wa Viti Maalum (Chadema) akifurahia Kombe la Kagame kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma... |
Wachezaji wa Yanga wakishangilia taji lao la ubingwa wa Kombe la Kagame hivi karibuni... kombe hilo limetambulishwa kwa wabunge mjini Dodoma leo |
Kikosi cha klabu ya Yanga kimetua kwa kishindo ndani ya Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo na kuibua shangwe na nderemo kutoka kwa
wabunge mashabiki wa timu hiyo wakati wakitambulisha kombe walilotwaa hivi
karibuni la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu Kombe la Kagame.
Baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu, wachezaji wa Yanga walioongozana na mwenyekiti Yusuf Manji, Makamu MwenyekitiClement Sanga, mjumbe wa bodi ya wadhamini, Mama Fatma Karume na Francis Kifukwe walitambulishwa na bungeni na kupongezwa na Spika wa Bunge, Mhe. Anna Makinda.
Kufuatia tukio hilo, wabunge
waliripuka kwa shangwe na bashasha tele, huku
wale ambao wanafahamika kuwa ni mashabiki wa Simba, kama Mhe. Ismail Aden Rage ambaye
pia ni mwenyekiti wa wekundu hao wa Msimbazi, wakionekana kushangilia vilevile,
lakini kwa namna ya utani zaidi.
Baada ya utambulisho wa msafara wa wachezaji wa Yanga, wakiwamo
nyota kama Haruna Niyonzima ‘Fabregas’, Hamis Kiiza na mfungaji bora wa michuano ya Kagame, Said
Bahanunzi, likaja tukio la kuonyeshwa kwa kombe walilotwaa, la Kagame.
Nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’ alisimama na kombe hilo, akaenda mbele na kulipunga
hewani huku akilielekeza kila upande ili wabunge wote wapate nafasi ya kuliona.
Ushangiliaji wa kupiga meza ulitwaa nafasi na kuufanya
ukumbi mzima urindime.
Hata hivyo, katikati
ya kushangilia huko, wabunge wengi ambao ni mashabiki wa Simba, wakiongozwa na Rage, wakajibu
mapigo ya wapinzani wao wa jadi kwa namna ya kuchekesha zaidi baada ya kunyoosha
juu vidole vitano vya mkono; pengine wakikumbushia matokeo
ya kichapo kikali cha mabao 5-0 walichowapiga Yanga katika mechi yao ya mwisho
ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara!
Baadaye, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe akawapongeza Yanga wakati akisoma hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka ujao wa fedha.
Membe ambaye pia ni mnazi wa Yanga, akasema kwamba atakuwa hajatenda haki kama hatawapongeza Yanga ambao wamekuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kutwaa ubingwa wa Kagame unaohusisha klabu bingwa za Afrika Mashariki na Kati; na kwamba amefurahi kuwa ujio wao bungeni umekuja katika siku mwafaka ambayo wizara yake inawasilisha bajeti ya mwaka ujao wa fedha.
Yanga walitwaa kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo baada ya kushinda 2-0 katika mechi yao ya fainali dhidi ya Azam FC.
No comments:
Post a Comment