Sunday, August 5, 2012

USAJILI WA MRISHO NGASSA SIMBA WAMUOKOA KABURU, MKUTANO WAMALIZIKA BILA MIZENGWE WALA FITNA...!!

Simba oyeee....! Makamu Mwenyekiti wa Simba, Godfrey Nyange 'Kaburu' akisalimia wanachama katika mkutano mkuu wa klabu hiyo uliofanyika kwenye Ukumbi wa Bwalo la Maafisa wa Polisi, Oysterbay jijini Dar es Salaam leo. 


Baadhi ya wanachama wa Simba wakifuatilia mkutano wao leo.
Straika mpya wa Simba, Mrisho Ngassa anavyoonekana wakati akiwa mazoezini na klabu yake ya Simba. Usajili wa straika huyu ndio unaodaiwa kumuokoa Kaburu leo.
Ngassa (mbele kushoto) akiwa mazoezini na wachezaji wenzake wa Simba. Usajili wa Straika huyu unadaiwa ndio uliomuokoa Kaburu dhidi ya kuibuliwa mizengwe leo.  
Straika Ngassa akiwa na 'mkoko' alioupata baada ya kukubali kutua Simba. 
Straika Ngassa akipokewa kwa mbwembwe na mashabiki wa klabu yake mpya ya Simba.  
Kaburu alipocheza kama Pele kwa kukamilisha usajili wa Ngassa na kumtambulisha 'fasta' mbele ya waandishi wa habari muda mfupi kabla ya mkutano mkuu.
Kaburu (kushoto) akiwa na straika wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Okwi, ambaye inadaiwa kuondoka kwake Msimbazi na kwenda kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa Ulaya nusra kutumiwe na mahasimu wa Kaburu ndani ya Simba kumng'oa kiongozi huyo leo. 

Ule mkutano mkuu wa kawaida wa wanachama wa klabu ya Simba uliodhaniwa kuwa utamng’oa Makamu Mwenyekiti Godfrey Nyange ‘Kaburu’ umemalizika kwa amani na bila zengwe lolote kwenye ukumbi wa Bwalo la Maafisa wa Polisi  Oyesterbay jijini Dar es Salaam.
Awali, kulikuwa na uvumi kuwa Kaburu angebanwa wakati wa kujadili ajenda ya ‘mengineyo’  kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni kuidhoofisha timu kwa kumuweka sokoni Straika wao nyota, Mganda Emmanuel Okwi na pia kufanya uzembe uliowapa mwanya mahasimu wao wa jadi, Yanga kumtwaa ‘kiulaini’ aliyekuwa beki wao ‘jembe’ kwa  nafasi ya kati, Kelvin Yondani.
Hata hivyo, mambo yalikuwa tofauti ukumbini kwani Kaburu ni miongoni mwa viongozi walioshangiliwa sana wakati wakizungumza, huku salama yake hiyo ikielezewa na baadhi ya wanachama wa Simba kuwa ni kufanikisha kwake usajili wa straika nyota wa timu ya taifa (Taifa Stars), Mrisho Ngassa ambaye wamemnasa kwa mkopo wa Sh. milioni 25 kutoka Azam.
“Kaburu amepona kwa sababu hakukuwa na sababu yoyote ya kumuanzishia zengwe la kumtoa. Usajili alioushughulikia kwa mafanikio wa mshambuliaji Mrisho Ngassa umezima kabisa jaribio la kumtingisha katika nafasi yake,”  amesema mmoja wa wanachama wa klabu hiyo.

Baada ya kumalizika kwa mkutano huo, mashabiki wa Simba waliondoka ukumbini na kujiandaa kwenda kutazama mechi ya ufunguzi wa michuano mipya ya Super 8 kati ya timu yao na Jamhuri ya Pemba inayofanyika jioni hii kwenye Uwanja wa Chamazi.

No comments:

Post a Comment