Monday, July 16, 2012

SOMA JINSI MCHUNGAJI GWEJIMA ALIVYOFUNGUKA AKIKANUSHA MADAI YA POLISI KWAMBA MTUHUMIWA WA UTEKAJI WA DKT. ULIMBOKA ALIENDA KUTUBU KANISANI KWAKE



Mchungaji Gwejima


Mchungaji Gwejima


Siku chache tu baada ya Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova kutangaza kuwa wanamshikilia raia wa Kenya Joshua Gitu Mhindi (31) kutokana na kuhusika kwake na tukio la kumteka na kumpiga Dk. Steven Ulimboka, ikiwa ni baada ya kukiri mwenyewe kuwa alihusika wakati akitubu kwenye Kanisa la Ufufuo na Uzima, Mchungaji Josephat Gwejima wa kanisa hilo lililopo Kawe jijini Dar es Salaam ameibuka na kutolea ufafanuzi suala hilo.

Mchungaji Gwejima ametoa ufafanuzi huo leo mbele ya mamia ya waumini wake wakati wa ibada ya Jumapili.

Mchungaji Gwejima alisema kwamba jana na juzi, watu wengi walimipigia simu kutaka ufafanuzi katika jambo linalowahusu. Kwamba alipigiwa simu kutoka ndani na nje ya nchi, kwa hiyo na yeye (Gwejima) ameona alifafanue jambo hilo kabla ya ibada.

Akasema kuwa Jeshi la polisi wiki hii lilitoa taarifa kwenye vyombo vya habari kwamba aliyemteka Dk.Ulimboka amekwenda kwenye Kanisa la Ufufuo na Uzima kutubu, akawa anamtafuta yeye (Mchungaji Gwajima), lakini akawa hakumpata na alipomkosa akampata Mchungaji Joseph Marwa na akatubu kwake.

Gwejima alisema kuwa alipata taarifa hizo kupitia BBC na vyombo vingine vya habari. Akasema jambo hilo likawaletea kanisani mambo manne.

Akaongeza kuwa kwanza, kwa tamaduni za kanisani, mtu akienda kutubu zile taarifa za toba yake huwa hazitakiwi kutangazwa, na hivyo ikaonekana kuwa katika Kanisa la Ufufuo, mtu amekwenda kutubu toba na yake ikasambazwa kwenye vyombo vya habari; jambo ambalo yeye hakulipenda.

Akasema kuwa jambo la pili, inaonyesha kuwa wachungaji wawili ndio waliokuwa wanatafutwa, ambao ni yeye (Mchungaji Gwajima) na pia Mchungaji Marwa. Akasema kuwa vilevile jambo hilo halikumpendeza kwasababu watu wengi hawakuwa na habari.

Jambo la tatu, akasema Mchungaji Gwejima kuwa kuna wingu zito la utata kati ya madaktari na serikali na hivyo taarifa hiyo ikataka kuleta picha kuwa Kanisa la Ufufuo na Uzima limeandaliwa kuisafisha serikali katika jambo hilo.

Mchungaji Gwejima akaongeza kuwa jambo la nne, ni kwamba watu wameshangazwa maana jambo hili lilikuwa halijawahi kutangazwa kwamba kuna mtu aliyehusika na kumteka Dk.Ulimboka.

Kutokana na hali hiyo, Mchungaji Gwejima akasema kuwa imembidi atolee ufafanuzi jambo hilo.
“Kwa hiyo nitafafanua, bahati mbaya itawafikia hata watu ambao hawakulengwa,” alisema.

Mchungaji Gwejima alisema ufafanuzi huo haulengi jamiii nyingine iliyo nje ya kanisa lake, bali unalenga mchungaji ambaye anataka kufafanulia waumini wake kuhusu taarifa za mtu ambaye alidaiwa alikwenda kutubu kwa kumteka Dk.Ulimboka.

Akaongeza kuwa kati ya Juni 26 au 27, walikuwa kwenye ibada ya kumuombea Dk.Ulimboka maana ailiona si vyema daktari kutekwa na hivyo wakalaani kwa pamnoja wale waliomteka na mgomo wa madaktari, pia wakailaani serikali kwa kuchelewa kulipatia ufafanuzi suala la mgogoro huo (wa madaktari).

Alisema kuwa walipomaliza kuomba, kwa mujibu wa walinzi wao, akatokea mtu ambaye aliomba kuonana na mchungaji kiongozi. Walinzi walisema hawezi akaonana naye mpaka shida yake awaeleze wao, lakini mtu huyo aliendelea kusisitiza, lakini hata hivyo walinzi hawakumruhusu na kumweleza kuwa kama ana shida awaeleze wao.
Walinzi hao walishikilia msimamo kuwa kama hataki kuwaeleza hatapata nafasi ya kwenda kumuona, hasa ikizingatiwa kuwa mtu mwenyewe alionekana wa ajabu ajabu, kichaa si kichaa, mtu mzima si mtu mzima.

Mchungaji Gwejima akaeleza zaidi kuwa walinzi walibaini huyo mtu si salama kwa jinsi alivyokuwa. Baadaye mtu huyo akasema ametokea Kenya na kwamba yeye ni Mkenya, na kwamba alikuwa na mambo mengi ya kumweleza mchungaji, yakiwemo ya kuwa yeye (huyo mtu) na wenzake wa kikundi fulani walihusika kumteka Dk.Ulimboka.

Akasema walinzi waliposikia hivyo, wakajua jambo hilo ni zito. Hata hivyo hawakuweza kumjulisha yeye (mchungaji kiongozi) kwasababu huwa wanakutana na watu wengi wa aina hiyo. Baada ya hapo, mtu huyo alianza kuelezea mambo mengi.

Mchungaji Gwejima akaendelea kueleza kuwa hata hivyo, walinzi walibaini mambo mengi, ikiwemo kwamba huenda mtu huyu hana akili timamu, hajui atendalo, ama mtu huyo ametumwa kwa lengo fulani au anayoyasema yana ukweli lakini walinzi hawakutaka kumjulisha.

“Nataka nisahihishe kauli ya kwamba alikuwa anataka kutubu… hapana, alikuwa anamtafuta mchungaji. Hata hivyo, kama alikuwa anatafuta kutubu, yeye ni Mkenya (na hivyo) angeenda Kenya, tena kwenye kanisa analosali kama anatafuta kutubu,” alisema Mchungaji Gwejima.

Hata hivyo, Mchungaji Gwejima akaeleza zaidi kuwa watu wa Mungu waliookoka hawana utaratibu wa kwenda kumuona mchungaji kutubu, utaratubu wa neno la Mungu likiwa linahubiriwa, unamuomba Mungu wewe mwenyewe na Mungu anakusikia.

“Ni kanisa katoliki pekee ambalo lina utaratibu wa kwenda kumweleza Padre au Paroko na kumweleza matatizo yako na kuyatubu, lakini makanisa yote ya Mungu yaliyookoka hayana utaratibu huo,” alisema.

Mchungaji Gwejima alisema kuwa mambo kadhaa yanayoweza kujitokeza katika suala hilo ni kwamba:

-Kwanza, inawezekana mtu huyo alitumwa hapo ili atokee katika kanisa hilo ambalo lina maelfu ya watu na hivyo jambo hilo liweze kusikika haraka.
- Pili, inawezekana mtu huyo ni mhalifu anayetembea hapa na pale kufanya uhalifu.
- Tatu, inawezekana ni kweli mtu huyo ameyatenda anaysema, lakini swali linakuja ni kama kweli ametenda hayo, kwanini aendelee kuwepo hapa nchini hadi sasa? Na kwanini aende kusema suala hilo katika kanisa la Ufufuo na Uzima?

Mchungaji Gwejima akaendelea kueleza kuwa kutokana na utata wa suala hilo, ilibidi mtu huyo abebwe msobe msobe na kupelekwa katika Kituo cha Polisi Kawe. Akasema kabla ya kupelekwa huko kituoni, mtu huyo alisema amepanga chumba karibu na Kituo cha Polisi Kawe na baada ya hapo, walizni walikwenda naye kwenye gesti hausi hiyo na kuchukua mikoba yake.

Baada ya kufikishwa kituoni, polisi waliwaeleza walinzi wa Kanisa la Ufufuo kwamba, kwa kuwa tayari wamekwisha mfikisha polisi, wamuache na hivyo walinzi wakaishia hapo.

Mchungaji Gwejima aliendelea kueleza kuwa wiki tatu zilizopita, polisi makao makuu walipiga simu kanisani hapo kutafuta walinzi waliomkamata Mkenya huyo, kwani mtu huyo alipopelekwa kituo cha Kawe akaulizwa kama ni kweli kuna maneno aliyoyasema pale kanisani ambapo alijibu ni kweli, hivyo polisi wakaamua kumpeleka kituo cha Oysterbay.

Akasema walinzi Joseph Marwa na Ernest walikwenda polisi ambapo walieleza kwamba mtu huyo alikwenda kanisani na kueleza jinsi mtu huyo alivyoeleza ambapo aliitwa mbele ya watu hao ambapo naye alidai kuwa kufahamu kuwa alikuja kwa ajili ya kumuona Mchungaji kiongozi.

“Kanisa la Ufufuo na Uzima tumekuwa mbele kusema ukweli,” alisema.

AKILI
Mchungaji Gwejima alisema kuwa mtu huyo, wakati akiendelea kuhojiwa, alipoulizwa kwanini anasema maneno hayo, alijibu kuwa ana matatizo ya akili na kwamba mapepo yakimwingia huwa anaropoka maneno hovyo. Mtu huyo alisema hayo mbele ya polisi, kwamba ana matatizo ya kuropoka hata kama maneno hayo hayana ukweli. Alipiga magoti mbele ya polisi na walinzi wa kanisa la Ufufuo kuomba asamehewe kwasababu ana tatizo la kuropoka na kusema mambo ambayo hata kama hayapo.

Akasema kutokana na maelezo hayo, polisi na walinzi walianza kujadiliana maneno hayo, ambapo walinzi walitoa ushauri suala hilo liishie hapo kanisani kwa sababu amesema ana tatizo la kuropoka. Walikubaliana, na polisi walikubali.

Akasema siku mbili baadaye, Kova alitangaza kupitia vyombo vya habari kwamba kuna mtu wamemkamata, aliyekwenda katika Kanisa la Ufufuo kuonana na Mchungaji Kiongozi kwa lengo la kutaka kutubu na kwamba alipomkosa alimkuta mchungaji Marwa na akatubu.

“Jambo hili limenishangaza sana kwasababu polisi na walinzi walikuwa wameshakubaliana suala hilo liishie hapa,” alisema.

 Akasema kuwa hata hivyo, polisi wao wana akili za kipolisi, siyo kama wachungaji inawezekana pamoja na kwamba mtu huyou alisema hana akili lakini inawezekana ni janja yake.

Alisema kuwa anachokilaani ni kitendo cha polisi kutangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mtu huyo alikwenda kutubu katika kanisa la Ufufuo wakati hakwenda kanisani hapo kutubu bali alikwenda kumtafuta mchungaji kiongozi. Kwa maana hiyo kanisa lake haliwezi kukubali suala hilo, akiamini kwamba limekuja kwa lengo la kuvuruga kanisa la Ufufuo.

Aliongeza kuwa Polisi hawakuwa sahihi kumtangaza mtu aliyedai amekwenda kutubu kanisani halafu wakamtangaza kwenye vyombo vya habari hali inayoonesha kana kwamba viongozi wa kanisa hilo hawana maadili.

Alisema kosa jingine ni la polisi ni kwamba hata kama ni kweli mtu huyo alikwenda kutubu lakini si haki kumtangaza kwenye vyombo vya habari.

Aliongeza kuwa kama mtu huyo alimteka au hakumteka Dk.Ulimboka suala hilo halilihusu kanisa la Ufufuo. Pia akasisitiza kwamba hakwenda kutubu kwao bali alitaka kumuona mchungaji kumweleza mambo gani au angemdhuru. Kanisa halina mashiko kwenye jambo hilo.

Alisema Polisi wamefanya vizuri sana kumkamata kwa sababu hata kama ni kichaa cha kwanza ni kumkamata na akawashauri kwanza kabla hawamjafanya wampime akili mtu huyo ili kubaini kama ana akili sawa.

Pia akakumbushia kuwa katika mgogoro huo wa madaktari na serikali kuna mtu ambaye ametajwa na jamii anayeitwa Hemed Msangi ambaye uvumi umeenea kuwa Dk. Ulimboka alimtambua na kwenye Bunge kuna mbunge alielezea jambo hilo hivyo akaliomba Jeshi la Polisi limkamate Msangi kwani hiyo itawasaidia kuondoa wingu lililopo nchini badala ya kumng’ng’ania mtu huyo.

Alisema mtu anayeshikiliwa ni mdogo sana kulinganisha na alivyotajwa Hemed Msangi na kwamba kuna watu wanapenda mgogoro huo uendelee kwa sababu hawana cha kupoteza lakini wao kanisa la Ufufuo wanacho cha kupoteza.

Aliongeza kuwa suala la serikali kuwafutia leseni madaktari halifai wakati imewasomesha kwa miaka sita.

Aidha, alisema wanaomshauri Rais wapo ambao hawajui namna ya kumshauri na kwamba yeye anamfahamu sana Mhe. Rais kuwa ana dhamira njema na Tanzania lakini ana wasiwasi na wanaomshauri kwamba wanamshauri ushauri usiofaa kwasababu katika hotuba ya Rais aliongea mambo mengi ambapo alisema wanatuhumiwa katika kumteka Dk.Ulimboka na serikali ni moja wapo hivyo ni bora serikali isiwe sehemu ya upelelezi wa tukio hilo.

Alitaka iundwe tume huru ya kuchunguza suala hilo akisema ni vyema isifanywe na polisi hao hao wanaotuhumiwa ili kuondoa wingu lililopo.



No comments:

Post a Comment