Thursday, July 26, 2012

MAITI MV SKAGIT ZAFIKIA 123, LEO ZIMEPATIKANA MAITI 17 ZIKIWEMO TANO ZILIZOKUTWA ZIKIELEA BAGAMOYO


Zoezi la kuopoa miili zaidi ya watu waliokufa katika ajali ya kuzama kwa boti ya Mv Skagit Zanzibar bado limekuwa likiendelea
Idadi ya miili ya watu waliokufa baada ya kuzama kwa boti ya Mv Skagit katika eneo la Chumbe visiwani Zanzibar wakati ikitokea jijini Dar es Salaam wiki iliyopita sasa imefikia 123 baada ya miili mingine 17 kupatikana leo.

Taarifa zimeeleza kuwa katika miili iliyopatikana leo, wapo wanaume 13 na wanawake wanne, huku mmoja kati yao akiwa ni binti wa miaka 15.

Imeelezwa zaidi kwamba miili ya watu watano kati ya hao ilipatikana katika fukwe za Bagamoyo mkoani Pwani na tayari imeshazikwa wilayani humo.

Boti ya Mv Skagit inayomilikiwa na kampuni ya Seagull Sea Transport Company Limited ilipata ajali Julai 18 katika eneo la Chumbe visiwani Zanzibar, mishale ya saa 7:00 mchana huku ikiwa na watu zaidi ya 340.

Inadaiwa kwamba ilikumbwa na tukio hilo baada ya kupigwa na dhoruba kali, kupinduka na kisha kuzama yote baharini.

Juhudi za kuifikia boti hiyo ili kupata miili zaidi ya watu wanaoweza kuwa walinasia ndani yake zinaelezwa kuwa ngumu kwani imezama chini kabisa kwa umbali unaokadiriwa kuwa ni wa kina cha zaidi ya mita 60 wakati uwezo uliopo ni wa binadamu kuzamia kwa kina cha mita 30 pekee.




No comments:

Post a Comment