Friday, July 6, 2012

16 BORA COPA COCA-COLA KUANZA J’MOSI

16 bora ya michuano ya Copa Coca-Cola 2012 inaanza kesho (Julai 7 mwaka huu) kwa mechi nne zitakazokutanisha timu nane kati ya 16 zilizofuzu hatua hiyo. Mechi hizo za 16 bora zitachezwa kwenye viwanja vya Kumbukumbu ya Karume na Tanganyika Packers vya Dar es Salaam.

Ruvuma iliyoongoza kundi A itacheza na Temeke iliyoshika nafasi ya tatu kundi C. Mechi hiyo itaanza saa 2.30 asubuhi Uwanja wa Karume. Mechi nyingine ya asubuhi itakayochezwa Tanganyika Packers itawakutanisha washindi wa pili kundi A Kigoma dhidi ya Mara walioshika nafasi ya nne kundi C.

Mechi za jioni kwa kesho zitakazoanza saa 10 kamili jioni zitakuwa kati ya Mjini Magharibi na Kagera kwenye Uwanja wa Karume wakati Morogoro na Pwani zitaumana kwenye Uwanja wa Tanganyika Packers ulioko Kawe, Dar es Salaam.

Hatua ya 16 bora itakamilika keshokutwa (Julai 8 mwaka huu) kwa mechi za asubuhi kati ya Kinondoni na Rukwa kwenye Uwanja wa Karume, na Dodoma dhidi ya Arusha kwenye Uwanja wa Tanganyika Packers. Mechi za jioni siku hiyo ni kati ya Kilimanjaro na Mwanza (Uwanja wa Karume) na Tabora na Tanga (Tanganyika Packers).

Timu zitakazoshinda zitaingia hatua ya robo fainali itakayochezwa Julai 10 na 11 mwaka huu kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume. Nusu fainali itachezwa Julai 13 mwaka huu, na kufuatiwa na mechi ya mshindi wa watatu na fainali ambazo zote zitachezwa Julai 15 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment