Saturday, June 30, 2012

MANCINI: NILIJUA BALOTELLI ANGEFUNGA MABAO MAWILI

Wee mkali, ila acha mapepe.... kocha Mancini (kulia) akimpa nasaha Balotelli katika mechi mojawapo ya klabu yao ya Manchester City


MILAN, Italia
KOCHA wa Manchester City, Roberto Mancini amemwagia sifa Mario Balotelli baada ya kuonyesha kiwango cha juu na kufunga mabao yote yaliyoipa timu ya taifa ya Italia ushindi wa mabao 2-1 katika nusu fainali yao ya Euro 2012 dhidi ya Ujerumani  juzi Alhamisi.
Siku zote Balotelli amekuwa akichukuliwa kuwa ni mchezaji mtukutu kwa sababu ya tabia yake ya kujiingiza kirahisi katika migogoro isiyokuwa na msingi ndani na nje ya uwanja. Hata hivyo,  Mancini, ambaye alimfundisha wakati akiwa Inter Milan na baadaye akamsajili Man City, hajawahi kumkatia tamaa mshambuliaji huyo mwenye miaka 21 na ameendelea kuamini kwamba ipo siku ataimarika kifikra na kutambua kipaji chake.
"Kwakweli amenifurahisha," kocha huyo Muitalia aliliambia Gazzetta dello Sport.
" Ni wakati ambao anaweza kuupita na kubadilika kutoka kuwa mchezaji mzuri na kuwa mchezaji nyota.
"Na dhidi ya Hispania katika fainali Jumapili, natumaini kwamba ataibeba timu. Wakati wake wa kujijengea heshima umewadia."

Mancini alisema vilevile kwamba alijua mapema kuwa Balotelli angefunga mabao mawili dhidi ya Ujerumani, ingawa hakufurahishwa na kitendo cha mshambuliaji huyo cha kujipa kadi ya njano kizembe kufuatia shangilia yake ya kuvua baada ya kupachika goli ‘kali’ la pili.

"Ilionekana wazi kwamba Mario angefunga mabao mawili; nilijua tu," mchezaji huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Italia alisema.
 "Nilijua kuwa ule ulikuwa ni usiku wake na kwamba ndiye ambaye angeleta tofauti ya mechi.

"Nilifikiria nini baada ya goli lake la pili? Ni kwamba angeweza kufunga bao jingine. Lakini ni aibu kwamba alivua jezi. Asingeruhusu kulimwa kadi ya njano."
Italia sasa watakabiliana na Hispania katika mechi itakayochezwa mjini Kiev kesho na kumpata bingwa wa Euro 2012, mechi ikitarajiwa kupigwa kesho Jumapili kuanzia saa 3:45 (kwa saa za Afrika Mashariki)

No comments:

Post a Comment