Thursday, November 28, 2013

WAKONGWE KIBAO WAPANIA KUSHIRIKI TAMASHA LA GURUMO DESEMBA 14


MKONGWE wa muziki wa dansi Kassim Mapili amethibisha kushiriki Tamasha la Gurumo 53 litakalofanyika Jumamosi ya tarehe 14 mwezi Disemba mwaka huu.

Mapili amesema si yeye tu, bali pia ataratibu mpango mzima wa kuhakikisha wakongwe wote wa muziki wa dansi wanashiriki tamasha hilo bure bila malipo yoyote.

Tamasha hilo ambalo ni mahsusi kwaajili ya kumuaga mwimbaji mkongwe Muhidi Maalim Gurumo litafanyika Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya TCC Club Chang’ombe.

Mratibu wa tamasha hilo, Juma Mbizo amesema Mapili ameamua kubeba jukumu la kuandaa wakongwe ambao ambao watatengeneza wimbo maalum wa kumuaga Gurumo utakaosikika kwa mara ya kwanza TCC Club Disemba 14.

Baadhi ya wakongwe  wengine waliothibitsha kushiriki Tamasha la Gurumo 53 ni pamoja Komandoo Hamza Kalala, Tshimanga Kalala Assossa na Waziri Ali.

Gurumo anaagwa kufuatia  kutangaza kwake kuachana rasmi na muziki wa jukwaani baada ya kudumu kwenye kazi hiyo kwa miaka 53.

Bendi za Twanga Pepeta, Msondo Ngoma na wanamuziki kibao waliowahi kung’ara na Sikinde ni sehemu ya wasanii watakaosindikiza tamasha hilo linalosubiriwa kwa hamu.

Hadi kustaafu kwake Gurumo aliyezitumikia pia bendi za Kilimanjaro Chacha,Rufiji Jazz, Kilwa Jazz, Sikinde na OSS – Ndekule, alikuwa ni kiongozi na mmoja wa wamiliki wa Msondo Ngoma.

Wasanii waliowahi kuitumikia Sikinde ambao watakuwepo kumsindikiza Gurumo ni pamoja na Cosmas Chidumule, Abdallah Gama, Hussein Jumbe, Mashaka Shaaban, Kalamazoo, Henry Mkanyia na Karama Legesu. Wengine ni Ali Yahaya na Boniface Kachale, Benno Villa Anton, na Ibrahim Mwinchande.

Hata hivyo, licha ya wasanii hao waliowahi kuitumikia Sikinde kuwemo kwenye tamasha hilo, bendi ya Mlimani Park “Sikinde Ngoma ya Ukae” haitashirki katika Gurumo 53 kutokana sababu zilizo nje ya uwezo wao.

Mbizo amesema Mlimani Park ina mkataba unaowabana kufanya onyesho lolote litakalowakutanisha na Msondo hadi baada ya sikukuu ya Krismasi (Disemba 25, 2013).

Juma Mbizo amesema licha ya Sikinde kutoshiriki tamasha hilo lakini nyimbo zote zilizotamba ndani ya bendi hiyo ambazo zilitungwa na Gurumo, zitarindima TCC Club kwa ubora ule ule.

“Wanamuziki wengi waliofanya kazi na Gurumo katika Sikinde enzi hizo, hawako tena katika bendi hiyo, hivyo watakuwa huru kuungana na mwimbaji huyo mkongwe na kushusha burudani nzito.

No comments:

Post a Comment