Thursday, July 26, 2012

SOMA TAARIFA MPYA KWA WANACHAMA WA MIFUKO KUHUSU FAO LA KUJITOA


TAARIFA KWA UMMA KUHUSU KUSITISHWA KWA FAO LA KUJITOA

Irene Isaka, Mkurugenzi wa SSRA
Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), inapenda kutoa ufafanuzi juu ya mafao ya kujitoa. Ufanunuzi huu unakwenda sambamba na taarifa mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa na vyombo vya habari na kuleta mkanganyiko miongoni mwa Wanachama na Wadau wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii.

Kufuatia hali hiyo, Mamlaka inatoa ufafanuzi ufuatao:
-   Marekebisho kuhusu kusitisha fao la kujitoa yamefanyika ili kutimiza lengo na madhumuni ya Hifadhi ya Jamii ambayo ni kuhakikisha kuwa mwanachama anapostaafu anapata mafao bora yatakayomwezesha kumudu hali ya maisha uzeeni.
-     Ni kweli kuwa Sheria za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii pamoja na Sheria ya Mamlaka zimefanyiwa marekebisho. Mchakato wa marekebisho hayo ulihusisha wadau kwa kuzingatia utatu yaani wawakilishi kutoka Vyama vya Wafanyakazi, Chama cha waajiri pamoja na Serikali.
-     Kwa kutambua tofauti ya ajira, tofauti ya mazingira ya kazi, tofauti ya sababu za ukomo wa ajira, na umuhimu wa Mwanachama kunufaika na michango yake wakati angali katika ajira, Mamlaka inaendelea na mchakato wa kuandaa miongozo na kanuni za mafao ambazo lengo lake ni kuboresha maslahi ya Wanachama. Miongozo na kanuni hizo zitajadiliwa na Wadau wakiwemo Wafanyakazi, Waajiri na Serikali kabla ya kuanza kutumika.

-    Kufuatia kuanza kutumika kwa Sheria hiyo maombi mapya ya kujitoa yamesitishwa kwa kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo itakapotolewa ili kuiwezesha Mamlaka na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu kwa Wadau.

-    Tangazo hili halitowahusu Wanachama waliojitoa kabla ya tarehe 20/07/2012.
-   Mamlaka inakanusha vikali kwamba, sitisho la fao la kujitoa si kwa sababu za Kiserikali au kwa sababu mifuko imefilisika. Tunapenda kuwahakikishia kwamba Mifuko yote ipo thabiti na michango yote ya Wanachama ipo salama.

-    Hivyo, Mamlaka inawaomba Wanachama na Wadau wote wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii kuwa na utulivu wakati mchakato huu ukiendelea kwa lengo la kulinda na kutetea maslahi ya Mwanachama.

Imetolewa na kitengo cha Mawasiliano na Uhamasishaji
SSRA-Makao Makuu

No comments:

Post a Comment