Thursday, June 21, 2012


CHINA WAJIANDAA KUMPOKEA DROGBA

Drogba akiwa na kombe la Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya


SHANGHAI, China
WAKATI  wachezaji wa Shanghai Shenhua wakijiandaa kucheza na mchezaji mwenzao mpya, Didier Drogba, kocha wao Sergio Batista alisema anakaribia kumnasa mchezaji mwingine wa kimataifa wa Colombia, Giovanni Moreno ili kuipa nguvu timu yao inayohaha katika ‘Chinese Super League’, Ligi Kuu ya China.
Drogba ambaye ni mshambuliaji wa timu ya taifa ya Ivory Coast, alitangaza kwamba amekubali kusaini mkataba wa kuichezea Shanghai kwa miaka miwili na nusu juzi, lakini badala ya kuridhika na usajili huo, Batista ambaye ni kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Argentina ameendelea kufukuzia mchezaji mwingine mwenye jina kubwa.
Moreno ( 25), ambaye hivi sasa anaichezea klabu ya Racing ya Argentina, ametajwa kuwa ni mchezaji sahihi wa kumsaidia Drogba na Batista alisema kuwa anatarajia kiungo huyo mshambuliaji atatua China kabla ya mwisho wa mwezi.
"Pengine bado kuna vikwazo kutoka katika klabu ya Moreno. Natarajia kwamba atatua Shanghai wiki hii au wiki ijayo," kocha huyo aliwaambia waandishi wa habari kwenye mkutano wa kila wiki wa klabu yake na waandishi wa habari jana.
Shanghai walisema kwamba ndoto yao imekuwa kweli wakati wakithibitisha kumsajili Drogba na kwamba mshambuliaji huyo anaweza kushirikiana katika kushambulia na mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Ufaransa, Nicolas Anelka.
Drogba ataungana na wenzake Julai baada ya mkataba wake na Chelsea kumalizika na Batista ana shauku kubwa ya kuwa na mshambuliaji huyo mwenye nguvu, anayefahamika pia nchini China kwa jina la 'The Beast'.

KUPANDA KIWANGO
Wakati uhamisho wa Drogba, ulioripotiwa kuambatana na masharti ya mshahara wa dola za Marekani 300,000 (Sh. milioni 500) kwa wiki ukiwa gumzo duniani, baadhi ya mashabiki nchini China wamekerwa kuona kwamba fedha nyingi zinalipwa kwa mchezaji mmoja tu na sio kuwekezwa katika kuwaendeleza vijana kwa ajili ya timu ya taifa.
Hata hivyo, beki wa Shanghai, Dai Lin anaamini kwamba kuwasili kwa Drogba kunaweza kuwasaidia katika kukuza viwango vyao.
"Uhamisho wa Drogba ni mzuri kwa timu yetu na kwa soka la China," Dai aliwaambia waandishi wa habari.
"Tuna mengi ya kujifunza kwa nyota wa kimataifa kama yeye, ikiwa ni pamoja na weledi na ujuzi wa soka. Na zaidi ya yote, Drogba ni mchezaji ambaye ameshatwaa taji la Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya."
Wachezaji wa Shanghai na mashabiki wao watakuwa na matumaini kwamba Drogba, aliyefunga penati iliyoisaidia Chelsea kuifunga Bayern Munich na kutwaa ubingwa wa Ulaya mwezi uliopita, anaweza kuibeba mara moja baada ya timu hiyo kuanza msimu vibaya.
Shanghai wanakamata nafasi ya 12 katika msimamo wa ligi wenye timu 16 ikiwa ni baada ya kuanza vibaya katika mechi 13. Batista ni kocha wao wa tatu msimu huu baada ya kuwatimua mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Ufaransa, Jean Tigana na kusitisha kipindi kifupi cha uongozi wa muda wa Anelka, licha ya kusudio la mshambuliaji huyo kutaka kuendelea na kibarua hicho.
"Kila mmoja katika timu yetu amefurahi sana kwa sababu tumekuwa tukitarajia tangazo hili kwa muda mrefu," alisema kiungo wa Shanghai, Yu Tao.

No comments:

Post a Comment