Wednesday, June 20, 2012

Club E kuleta Hollywood ndani ya Dar

Mwanamuziki wa DRC, Fally Ipupa (katikati) akishambulia jukwaa wakati alipokuja nchini na kutumbuiza katika Club E.

KWA mara nyingine tena, Embassy kupitia chapa yake ya Club E inakuja na pati ya aina yake inayojulikana kama Hollywood Glam Night. Ni Pati ya kipekee itakayoleta mandhari ya Hollywood jijini Dar es salaam. Pati hii ya aina yake itafanyika Ijumaa hii tarehe 22 katika ukumbi wa Blue Pearl ulioko Ubungo Plaza kuanzia saa mbili usiku.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Tumaini Toroka, Meneja wa Sigara ya Embassy, pati hii yenye maudhui ya Hollywood itakuwa ya kwanza jijini Dar es Salaam ambapo wanachama na wapenzi wa burudani watapata wasaa wa kuona burudani mbalimbali na vivutio vya mandhari ya Hollywood ambazo zimeandaliwa mahsusi kwa ajili ya wanachama wa Club E.

Wanachama wa Club E wataingia bure kwenye pati hii kwa kupitia mwaliko maalum wakati watu wengine ambao si wanachama wa Club E watalipa Sh.30,000 tu za Kitanzania. Kiingilio hiki kitajumuisha vinywaji pamoja na chakula.

Kwa miaka mitano iliyopita, Club E imejijengea jina kwa kufanya pati zenye ubora na hadhi ya hali ya juu kwa wanachama wake. Ukiacha suala la kuburudisha wanachama wake, kwa kipindi cha miaka mitano Club E pia imetoa mchango wake kwa kuinua wanamuziki wetu wa ndani ambao wamepata wasaa wa kuimba kwenye jukwaa moja na wasanii mbalimbali wa bara la Afrika na Marekani.

Club E ilianzishwa mwaka 2007 kwa lengo la kuwaleta pamoja na kuwaburudisha wanachama wake ambao ni wavutaji wa sigara ya Embassy. Tangu kuanzishwa kwake Club E imefanya pati nyingi na kuwaleta wasanii wengi wa ndani na nje ya nchi kutumbuiza. Wasanii walioletwa Club E ni pamoja na Werrason, Miriam Makeba, Amani, Blue 3, Lady Jay Dee, Mbilia Bell, Tshala Muana, JB Mpiana, FM Academia, Chaka Khan na Fally Ipupa.

Wanachama wa Club E wategemee pati ya aina yake Ijumaa hii na tunahimiza wasikose kuja kushuhudia pati hii itakayokuwa ya kipekee itakayosheheni burudani mbalimbali. Kwa ambao si wanachama wa Club E tiketi zinapatikana Steers mjini, Engen Petrol Station Mbezi, Mile PambaMwenge, Club Maisha Oysterbay, Steers Kijitonyama na TCC Club Chang’ombe.

No comments:

Post a Comment