Tuesday, October 30, 2012

NSA JOB AFUNGWA HOGO MGUU ULIOVUNJIKA

Mshambuliaji wa Coastal Union, Nsa Job, akivunjika goti akigongana na kipa wa JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Chamazi Jumapili Oktoba 28. 2012. Coastal ilishinda 3-0.
Madaktari wakimsaidia Nsa Job baada ya mguu kuhama kutoka kwenye maungio yake ya goti

Nsa Job akiugulia wakati akipelekwa kwenye gari la wagonjwa tayari kwa safari ya kelekea hospitalini Muhimbili

Nsa Job akiugulia baada ya kufikishwa hospitalini. PICHA ZOTE: Kwa hisani ya Gazeti la MWANANCHI

MSHAMBULIAJI wa timu ya Coastal Union ya Tanga, Nsa Job, ambaye alivunjika mguu baada ya kugongana na kipa wa JKT Ruvu juzi wakati timu hizo zilipokutana katika mchezo wa Ligi Kuu ya Bara uliofanyika kwenye Uwanja wa Chamazi amefungwa plasta ngumu na atakosa mechi zote tatu za mzunguko wa kwanza wa ligi zilizobakia.

Kwa mujibu wa taarifa zilizoandikwa kwenye tovuti ya klabu hiyo na mkurugenzi wa timu hiyo, Nassor Bin Slum, baada ya vipimo kuonyesha kuwa goti la mshambuliaji huyo liligeuka, madaktari wa hospitali ya Taifa ya Muhimbili (Moi) walifanikiwa kulirejesha katika hali ya kawaida na kumfunga plasta ngumu ili kuufanya urejee kwenye hali ya awali.

Taarifa hiyo inaongeza kuwa baada ya kupatiwa tiba hiyo, mchezaji huyo aliruhusiwa kurejea katika kambi ya timu hiyo ambayo inajiandaa na mechi yake dhidi ya Azam itakayofanyika kesho kwenye Uwanja wa Chamazi.

"Alhamdulillah ule wasiwasi tuliokuwa nao mwanzo baada ya Nsa Job kuumia sasa niseme umepungua kwani baada ya kumfikisha hospitali na kupigwa X-ray ilionekana tatizo ni 'dislocation of joint' (viungo kupishana katika maungio) na madaktari wamefanya kazi ya ziada kulirudisha goti lake katika sehemu yake na ameshafungwa POP, na hivi sasa amerudi kulala hotelini na wenzake. Inshaallah apone haraka aje kutimiza malengo aliyojiwekea " alisema Nassor katika taarifa aliyoitoa.

Mechi nyingine atakayoikosa mshambuliaji huyo aliyeisaidia timu yake kushika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ni dhidi ya Polisi Morogoro na dhidi ya mabingwa wa mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), Yanga ambayo ni ya kufunga mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo itakayofanyika Novemba 11 jijini Tanga.

Daktari wa Coastal Union, Dk. Francis Mganga alisema hali ya kiungo wao Mkenya Jerry Santo aliyeumia pia katika mechi hiyo ya juzi ni mbaya na hawatarajii acheze katika mechi zilizobaki za mzunguko wa kwanza na kwamba mchezaji Joseph Malubo pia ni majeruhi wa uvimbe wa goti.

No comments:

Post a Comment