Wednesday, July 18, 2012

FREDERICK MWAKALEBELA ASAKWA NA TAKUKURU


Fredrick Mwakalebela

Mkurugenzi wa Takukuru, Dk. Edward Hosea
Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Frederick Mwakalebela anasakwa kwa udi na uvumba na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) ili afikishwe mahakamani kukabiliana na kesi inayomkabili ya kudaiwa kutoa rushwa wakati akiwania kupitishwa kuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Iringa Mjini kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) wakati wa uchaguzi mkuu mwaka 2010.

Notisi iliyotolewa jana na Takukuru inamtaka Mwakalebela kutii wito wa kujisamilisha mwenyewe katika ofisi za Takukuru kabla hajakamatwa kwa mujibu wa hati ya mashitaka iliyoandaliwa.

Taasisi hiyo imefikia uamuzi huo baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa kutupilia mbali hoja mbili za kesi ya rufani dhidi ya Jamhuri, namba 13 ya mwaka 2010 iliyokuwa ikiiomba mahakama kuu kutolea uamuzi mapingamizi ya kisheria ambayo mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Iringa ilishindwa kuyatolea uamuzi na mengine kufanyiwa maamuzi kimakosa.

Stephen Mafipa ambaye ni Kaimu Kamanda wa Takukuru mkoa wa Iringa, amesema taasisi hiyo hivi sasa inamtafuta Mwakalebela popote pale alipo ili imfikishe upya mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili baada ya mahakama kuu kutupilia mbali rufaa hiyo.

Mwakalebela, aliyekuwa kinara wa kinyang’anyiro cha uchaguzi ndani ya CCM kabla ya kuenguliwa, alikata rufaa katika Mahakama kuu ya Tanzania, akipinga hati ya mashitaka iliyoandaliwa na jamhuri dhidi yake, akidai kwamba haitengenezi kosa la jinai kisheria kwa kuwa makosa yote yalivyotajwa.

Katibu huyo wa zamani wa TFF alihoji vilevile uhalali wa kifungu cha 21 (1) (a) na kifungu cha 24 (8) cha Sheria ya uchaguzi namba 6 ya mwaka 2010 ambacho ameshitakiwa nacho,akidai kwamba hicho pia hakitengenezi kosa la jinai kisheria.

Katika kesi ya msingi, Mwakalebela anadaiwa alitenda kosa hilo Juni mwaka 2010 katika Kijiji cha Mkoga, Manispaa ya Iringa ambapo anadaiwa kutoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Hamisi Luhanga ili azigawe kwa wapiga kura 30 wa CCM ili wampigie kura za maoni za kumchagua Agosti mwaka huo kuwa mgombea ubunge wa chama hicho.

Awali, akisoma hukumu hiyo ya kutupilia mbali hoja hizo, Jaji Rehema Mkuye alisema amezipitia hoja za pande zote mbili na kuona hoja ya kwanza ingekuwa na nguvu kisheria kama mashahidi wangekuwa wameitwa na kisha kutoa ushahidi wao.

No comments:

Post a Comment